Ni hija ya kiekumene ya maisha ya kiroho inayosimikwa katika damu ya mashahidi
Baba Mtakatifu Francisko anamshukuru kwa namna ya pekee Patriaki Bartholomeo wa kwanza
pamoja na Sinodi ya Costantinopoli kwa kutuma ujumbe maalum kwa ajili ya maadhimisho
ya Siku kuu ya Watakatifu Petro na Paulo, miamba wa imani. Baba Mtakatifu ameyasema
hayo, Jumamosi asubuhi, alipokutana na kuzungumza na Ujumbe wa kiekumene kutoka katika
Kanisa la Kiorthodox la Costantinopoli.
Anasema bado anaendelea kuhifadhi moyoni
mwake kumbu kumbu ya matukio ambayo yaliwakutanisha na Kaka yake Bartholomeo wa kwanza
wakati wa hija yake ya kitume Nchi Takatifu, mahali alikozaliwa Yesu, kama sehemu
ya maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 tangu Patriaki Anathegoras na Papa Paulo VI
walipokutana na kusali, mwanzo wa hija ya majadiliano ya kiekumene inayoendelea hadi
leo hii ndani ya Kanisa.
Baba Mtakatifu Francisko anakumbuka kwa umakini mkubwa
walipokutana na kusali kwenye Kaburi Takatifu, kwa kugusa msingi wa imani yao kwa
Kristo na Kanisa lake, hija ambayo ilihitimishwa kwenye kaburi la Mtakatifu Petro
mjini Vatican kwa kusali ili kuombea amani na upatanisho huko Mashariki ya Kati, tukio
ambalo liliwashirikisha Marais wa Israeli na Palestina. Matukio yote haya ni neema
ya Mungu, iliyowawezesha kukutana na kusali, ili kuonjesha upendo wa Kristo unaowaunganisha
pamoja pamoja na kuendelea kuonesha utashi wa kutaka kusonga mbele katika hija ya
majadiliano ya kiekumene ili kuweza kufikia umoja kamili.
Baba Mtakatifu anasema,
umoja miongoni mwa Wakristo ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu pamoja na nguvu na
neema ya Roho Mtakatifu inayowawezesha kuangaliana kwa macho ya kiimani, ili kujitambua
mintarafu mpango wa Mungu wa milele yote na wala si kwa yale yaliyojitokeza katika
historia ya maisha ya Kanisa na dhambi zilizowapelekea hadi wakafika hapo walipofikia.
Ikiwa kama Wakristo watajifunza kujiachilia mikononi mwa Roho Mtakatifu ili
awaongoze, daima wataendelea kuangalia katika "miwani" ya Mwenyezi Mungu, kwa kutembea,
kushirikiana na kutenda kwa umoja katika medani mbali mbali za mambo yanayowaunganisha
hadi wakati huu.
Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, mtazamo huu wa kitaalimungu
unarutubishwa na imani, matumaini na mapendo; una uwezo wa kutoa tafakari ya kina
kuhusu elimu ya Mungu "Scentia Dei", kwa kushiriki mtazamo wa Mungu alionao juu yao.
Ni tafakari inayoweza kuwasaidia kukaribiana zaidi katika umoja hata kama wanatoka
katika mielekeo tofauti.
Baba Mtakatifu anasema anaendelea kusali kwa ajili
ya mafanikio ya Tume mchanganyiko ya kimataifa katika mchakato wa majadiliano ili
kuendelea kufanya tafakari hii kwa kupiga magoti. Ni Tume inayoangalia umuhimu wa
Sinodi, Umoja wa Kanisa la Kiulimwengu na Utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro; tema
ambazo hazipaswi kubakia zinakumbatiwa katika masuala ya wasomi na kinzani, bali Wakristo
wanapaswa kuonesha ujasiri na imani kwa kazi ya Roho Mtakatifu, kwa kumpatia nafasi
ya kuliangalia Kanisa ambalo ni mchumba wa Kristo, anayetembea katika hija ya kiroho
ya kiekumene, inayoimarishwa kwa njia ya mashahidi walioyamimina maisha yao kwa kumuungana
Kristo na hivyo, kujenga majadiliano ya kiekumene kwa njia ya damu yao.
Baba
Mtakatifu Francisko amewashukuru wajumbe wa Kiekumene kutoka Costantinopoli, kwa heshima,
urafiki na upendo anapenda kwa mara nyingine tena kuwashukuru na kuwataka kumfikishia
salam na matashi mema, Patriaki Bartolomeo wa kwanza. Anawaalika kumwombea katika
maisha na utume wake. Baadaye kidogo, wajumbe hawa pamoja na Baba Mtakatifu Francisko
wamebadilishana zawadi.