2014-06-27 06:53:59

Ushuhuda wa maisha unatakiwa!


Katika maadhimisho ya Siku kuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu sanjari na siku ya kuombea utakatifu wa Mapadre iliyoanzishwa na Mtakatifu Yohane Paulo II kunako mwaka 2002. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI akatangaza na kuadhimisha Mwaka wa Mapadre kati ya Mwaka 2010-2011. RealAudioMP3

Bado kuna changamoto kubwa ya kuhakikisha kwamba, Mapadre wanakuza na kudumisha uaminifu wao kwa Kristo na Kanisa lake kwani Mapadre ni Watu wa Mungu kwa ajili ya Watu. Padre ni mhudumu wa Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa, ni mlezi wa Taifa la Mungu. Kanisa linawaalika waamini kuwaombea Mapadre kwani linatambua kwamba, zawadi hii kubwa imehifadhiwa kwenye vyombo vya udongo.

Askofu Augustino Shao wa Jimbo Katoliki Zanzibar anasema, Siku kuu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, sanjari na Siku ya kuombea Utakatifu wa Mapadre, Zanzibar kama Kanisa mahalia linapenda kusisitizia umuhimu kwa Mapadre kuwa wavumilivu, kuendelea kuwa Mashuhuda thabiti wa imani kwani Mapadre wakiyumba katika imani, amani inayotangazwa inaweza kutoweka pia. Mwaliko ni kwa Mapadre kuishi wito wao kwa kuendelea kuwa kweli ni mashuhuda katika medani mbali mbali za maisha!

Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mawosia yake ya kichungaji, anawataka Makleri kumwiga Yesu Kristo aliyejipambanua kwa kuwa ni kiongozi na mchungaji mwema; mwaminifu, mtiifu na mwenye huruma na mapendo pasi na mipaka. Hii ni changamoto na mwaliko kwa Mapadre kuhakikisha kwamba, wanamwiga na kumfuata Kristo katika uaminifu, upendo, unyofu, unyenyekevu, huruma na mapendo.

Mapadre wawe na mvuto na mashiko ili watu waweze kuonja huruma na upendo wa Mungu. Mapadre wawe ni mfano katika maneno na matendo yao kwa kumfuasa Kristo ambaye ni mfano bora wa utakatifu wa maisha, Bwana, Mwalimu na Mlezi wa Mapadre.







All the contents on this site are copyrighted ©.