Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 13 ya Kipindi cha Mwaka A wa Kanisa
Mpendwa msikilizaji wa kipindi tafakari masomo Dominika, niko pamoja nawe tena katika
Dominika hii ya XIII ya mwaka A, kukushirikisha furaha yangu toka meza ya Neno la
Mungu. Mwaliko toka Neno lenyewe ni kwamba mkristu aalikwa kuwa na upendo mkuu kwa
Mungu kuliko vitu vingine vyote.
Ni katika
kumpenda Mungu mkristu aweza kutoa huduma kwa wengine na kwa njia hiyo kuendelea kumpokea
Mungu zaidi na zaidi. Basi katika kutenda hayo Mungu anatangaza uhakika wa thawabu
kwa mwenye kutenda hilo.
Katika somo la kwanza toka kitabu cha Pili cha
Wafalme tunakutana na Nabii Elisha katika nchi ya Shunemu, pamoja na mwanamke mmoja
aliyekuwa mgumba lakini mwenye ukarimu na cheo! Mji wa Shunemu ulikuwa umejengwa kando
ya mlima na wakazi wake walikuwa wakulima ambao kwa njia ya kilimo walisadikika kujikusanyia
utajiri. Mara kadhaa Nabii Elisha alikuwa akipita mbele ya nyumba ya familia moja
ambayo haikuwa na mtoto. Kwa mazoea ya kupita pale mara kadhaa mama anaingiwa furaha
na kuitwa na ukarimu wa kimama na anamkaribisha chakulani Elisha.
Si hilo
tu bali mama huyu anamwomba mmewe ambaye alikuwa mzee wamtayarishie chumba mtumishi
wa Mungu huyu ili kila apitapo apate mahali pa kulala. Toka tendo hili la ukarimu
Mungu atamjalia mama huyu mtoto na hivi si tena mkiwa wala mgumba bali ukarimu umezaa!
Mama huyu anapomkaribisha Nabii Elisha anatangaza kwetu sisi namna ya ushiriki wake
katika mpango na kazi ya Mungu. Kwa ushiriki huu basi Mungu lazima atatoa zawadi nzuri
na hivi kujisikia mama mkamilifu.
Mpendwa msikilizaji tunapata kujifunza
kuwa, katika kuhudumia kuna baraka na heri za Mungu. Si hilo tu bali pia Elisha anatupa
picha ya kimisionari, yaani kuacha nchi yako na baadaye kukutana na familia nyingine
kubwa zaidi ndiyo Kanisa la Mungu. Kumbe hakuna haja ya kuogopa kunakotokana na kuacha
familia zetu kwa maana ni lazima Mungu atatoa tu kwa watenda kazi wake.
Katika
somo la Pili Mtakatifu Paulo anawaandikia Warumi akiwakumbusha maana ya ubatizo, yaani
ni kufa katika mauti ya Kristu na kufufuka naye. Baada ya ufufuko kama Bwana alivyo
mtakatifu, nasi tunaalikwa kuenenda katika upya wa maisha, yaani ule upya tulioupata
kwa njia ya Neema ya Utakaso. Ni katika mantiki hiyo ya ufufuko nasi tutaishi milele
pamoja na Kristu. Tunakuwa wapya kwa maana kwa njia ya ubatizo tunazika mambo ya kale
na kuanza maisha mapya.
Mpendwa msikilizaji, jambo la upya katika litrujia
ya ubatizo kwa sasa halionekani vizuri kama zamani ambapo mmoja alizamishwa katika
mto na hivi alipoibuka ilisadikika kwamba dhambi na mizigo ya zamani imechukuliwa
na mkondo wa maji. Kwa ubatizo maana yake tunakwenda pamoja na Kristu kaburini na
wakati anapofufuka tunatoka pamoja naye tukiwa wapya! Basi kama ambavyo Kristu harudi
tena katika mauti na mkristu vivyo hivyo hapaswi kurudi katika ukale wa maisha bali
anazaliwa upya na kuishi maisha mapya.
Katika Injili ya Matayo, Bwana anafundisha
namna mbatizwa ambaye amekufa katika mauti ya Bwana na kufufuka naye anavyopaswa kuishi
upendo. Upendo wake unapaswa kuwa wa kweli na sio wa kibaguzi, yaani upendo uliojaa
huduma kwa wengine. Namna ya kuishi mapendo haya ni kujitahidi kujibandua katika mgandamizo
wa tamaduni na hivi kuanza na Mungu kila siku safari ya upendo. Mpendwa, Upendo ambao
Bwana anautaka ni ule ambao unahudumu waliowahitaji na walio katika huduma ya Neno
la Mungu.
Mpendwa msikilizaji, Bwana akitaka kukamilsha hili, katika sehemu
ya kwanza ya Injili anasema, ni lazima anayetaka kunifuata na kuuishi upendo ajibandue
katika tamaduni na mizigo ya ndugu na mambo kama hayo na kuwa huru tayari kwa misioni.
Katika hili yawezekana kuona mbegu ya kukataa amri ya 4 ya Mungu! Bwana hayuko katika
mantiki hiyo yeye anachotafuta ni kwamba mfuasi lazima awe thabiti katika ufuasi wake
na si kubabaisha au kuwa nusunusu!
Katika sehemu II ya Injili, Bwana anakazia
suala la huduma kwa watenda kazi katika shamba lake. Anasema atendaye mema kwa hawa
watumishi anitumikia mimi. Hapa tunapata muunganiko pamoja na somo la kwanza pale
tunapomwona Elisha nabii akihudumiwa na familia moja huko alikokuwa akifanya utume
wake. Hata hivyo yafaa kuelewa vema jambo hili, yakwamba hoja kuu ni kushiriki katika
utume wa Mkombozi wa ulimwengu yaani Bwana wa mavuno mwenyewe.
Ninakualika
kushiriki kazi ya Bwana, maana ni kwa njia hiyo nawe unatayarisha neema na baraka
tele kama alizozipata mama mgumba aliyemhudumia Nabii Elisha katika somo la kwanza.
Ninakualika tena kuwa mtu ambaye unaweza kusifu na kukuza utukufu wa Mungu kwa njia
ya mapadre, masisita wanaohudumia taifa la Mungu popote duniani.
Kumbuka kuwaombea
hasa wale wanaofanya kazi katika nchi ambapo uhuru wa kuabudu umebanwa kwa asilimia
zote na hasa kwa kile kinachoitwa madhulumu ya kidini. Kwa kuwaombea utakuwa unashiriki
kikombe kimoja tukibarikisho kama ushirika wa Kristu na hivi kuwasaidia kujaliwa na
mastahili ya msalaba wa Bwana.
Nikutakie furaha na heri na hasa ukakue
katika moyo wa huduma kwa Kanisa na kwa familia yako na kisha mwisho wa maisha yako
hapa duniani upate uzima wa milele mbinguni. Tumsifu Yesu Kristu. Tafakari hii imeletwa
kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.