2014-06-27 08:42:18

Sayansi inaweza kuchangia kudumisha misingi ya haki na amani!


Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, sayansi inaweza kuwa ni chombo muhimu sana katika kukuza na kuendeleza misingi ya haki na amani duniani, kumbe, ni vyema na haki ikiwa kama watu wengi zaidi wataweza kufaidika na tafiti pamoja na majiundo makini ya kisayansi yanayotolewa duniani. Hii ni changamoto kubwa inayowahusisha wadau mbali mbali, lakini kwa namna ya pekee, wanasayansi na watalaam.

Ni changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 26 Juni 2014 alipokutana na kuzungumza na wanafunzi 25 kutoka katika Kituo cha Unajimu cha Vatican, kilichoko mjini Castel Gandolfo, nje kidogo ya mji wa Roma. Kituo hiki kilianzishwa kunako mwaka 1986, ili kutoa fursa kwa wanafunzi waliokuwa wanahitimu masomo yao kutoka kwenye Vyuo vikuu kunoa ubongo, kujenga na kudumisha urafiki na majaalimu pamoja na wanafunzi kutoka katika nchi ishirini na tatu. Ni fursa ya kujifunza kazi ya uumbaji na kwamba, wanayo kila sababu ya kuwashukuru wafadhili waliowawezesha kutimiza ndoto yao!

Baba Mtakatifu anasema, Kituo cha Unajimu cha Vatican ni mahali ambapo vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanajadiliana, wanashirikiana na kusaidiana kutafuta ukweli kuhusu nyota. Kanisa kwa upande wake pia linaendelea kufanya majadiliano na wanasayansi ili kuchangia katika tafiti mbali mbali kwa mwanga wa imani, kwa kutambua zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu amemkirimia mwanadamu na kwamba, anafurahia kuwaona watoto wake wakikua katika umri na hekima.







All the contents on this site are copyrighted ©.