Wingu la majonzi na simanzi limetanda mioyoni mwa Familia ya Mungu nchini Tanzania,
lakini kwa namna ya pekee kwa Waamini wa Jimbo Katoliki la Mbeya, kufuatia mauaji
ya kinyama aliyofanyiwa Sr. Crescentia Kapuli (52) aliyeuwawa kwa kupigwa risasi kifuani
na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi alasiri tarehe 23 Juni 2014 katika eneo la
River side, Ubungo, Jijini Dar Es Salaam alikokuwa anatekeleza utume wake kama mhasibu
wa Shule ya Sekondari na Chuo cha Ufundi cha Mwenyeheri Anwarite, Jimbo kuu la Dar
es Salaam.
Kwa masikitiko makubwa Sr. Immaculata Mirambo, Mama mkuu wa Shirika
la Watawa wa Bikira Maria Malkia wa Mitume, Jimbo Katoliki Mbeya, ambaye pia ni Mwenyekiti
wa Mashirika ya Kitawa Tanzania anasema, wamepokea msiba wa Sr. Kapuli kwa majonzi
makubwa, wanamwombea apumzike kwa amani na aendee kuwaombea watawa wenzake wasikatishwe
tamaa na changamoto na vitisho vya maisha, bali wamtumainie Mungu kwa kila jambo!
Ufuatao
ni wasifu wa Marehemu Sr. Crescentia Kapuli wa Shirika la Watawa wa Bikira Maria Malkia
wa Mitume Jimbo Katoliki Mbeya. Amezaliwa katika Kijiji cha Mkulwe, Wilaya ya Mbozi,
mkoani Mbeya, Agosti, 29, 1962 katika Kijiji cha mkulwe na kupata ubatizo Agosti,
31, 1962 huko Mkulwe na nambari ya cheti cha Ubatizo ni LB 19703, amepata Komunio
ya kwanza Oktoba,11, 1972 na kuimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara Oktoba, 12, 1972
huko huko Mkulwe.
Sr.Crescentia alikuwa ni mtoto wa mwisho kati ya watoto 12
wa Mzee Peter Kapuli na Mama Maria Nakana. Sr.Cresensia ameingia utawani kama mwomboaji
kunako mwaka 1979. Upostulanti mwaka 1980. Unovisi mwaka 1981 hadi mwaka 1983. Akafunga
nadhiri za kwanza tarehe 12 Desemba 1983 na baadaye kunako tarehe 12 Desemba 1991
akafunga nadhiri za daima. Tarehe 31 Mei 2009 akaadhimisha Jubilee ya miaka 25 ya
maisha yakitawa.
ELIMU Alipata elimu yake ya msingi katika shule ya msingi
Mkulwe mwaka 1972 hadi 1978, elimu ya Sekondari katika Shule ya Sekondari ya Bigwa
( Bigwa SR’s Secondary School) Mwaka 1994 hadi Mwaka 1997, amesoma chuo cha maarifa
ya nyumbani homecraft Mwanjelwa mwaka 1991 hadi mwaka 1992, amesoma Chuo cha Uhasibu
Mbeya na Dare Es salaam Mwaka 2000 hadi Mwaka 2002.
UTUME
Sr. Crescentia
amewahi kufanyakazi katika Convent ya Kyela akifanya Utume Parokiani mwaka 1984 na
kusimamia mradi wa mashine ya kusaga katika nyumba ya watawa iliyoko Mlowo mwaka 1985.
Msimamizi wa Jiko la Nyumba ya Utawala Jimbo Katoliki la Mbeya mwaka 1986 hadi mwaka
1989. Mlezi msadizi wa Wanafunzi wa Kitawa(Wanovisi) Mlowo mwaka 1993 hadi mwaka 1998.
Mlezi Msaidizi wa Wanafunzi wa Kitawa - Kisa Aspiranti Mwaka 1999 hadi mwaka 2000.
Utume
katika Convent Parokia ya Mwambani mwaka 2001. Utume Uaskofuni Convent akiwa Mama
Mkubwa wa nyumba na Mhasibu Jimboni Mbeya mwaka 2002 hadi 2009. Utume Gua Convent
akiwa Mama Mkubwa wa nyumba; Utume Parokiani na Mlezi wa Wawata 2009 – 2011.
Utume
Jimbo kuu la Dar es Salaam akiwa Mama Mkubwa katika Convent ya Makoka, Mhasibu Sekondari
ya Makoka na Chuo cha Ufundi cha Mwenyeheri Anwarite 2011 – 2014 hadi mauti yalipomfika.
Jimbo
kuu la Dar es Salaam, Alhamisi asubuhi tarehe 26 Juni 2014 wanaadhimisha Ibada ya
Misa Takatifu kwa ajili ya kumwombea na kumwaga Marehemu Sr. Crescentia Kaupili na
baadaye msafara utaondoka kuelekea Jimboni Mbeya. Taarifa za awali zinasema mara baada
ya kuwasili kwa mwili wa marehemu Sr.Cresensia utaingizwa katika makao makuu ya Shirika
la Bikira Maria Malkia wa Mitume, Jimbo Katoliki la Mbeya.
Baada ya kutoka
katika makao makuu ya Shirika safari itaanza kuelekea katika safari yake ya mwisho
hapa duniani Sr.Cresensia katika shamba la Mungu la Masista maeneo ya Hasamba, wilayani
Mbozi, mkoani Mbeya. Maziko yanatarajiwa kufanyika Jumamosi, tarehe 28 Juni 2014,
Mama Kanisa atakapokuwa anaadhimisha Siku kuu ya Moyo Safi wa Bikira Maria.
Raha
ya milele umpe ee Bwana na mwanga wa milele umwangazie apumzike kwa amani, Amina.
Taarifa hii imeandaliwa na Thompson Mpanji, Mbeya.