2014-06-25 11:30:57

Taka za plastiki ni balaa kwa ukuaji wa uchumi!


Taka za plastiki zinazoishia baharini zinasababisha uharibifu mkubwa wa mazingira kiasi hata cha kuhatarisha maisha ya viumbe hai baharini, utalii pamoja na sekta ya uvuvi. Haya yamebainishwa katika mkutano wa Umoja wa Mataifa unaoshughulikia mazingira uliofunguliwa rasmi tarehe 23 Juni na unatazamiwa kuhitimishwa hapo tarehe 27 Juni 2014.

Bidhaa ya plastiki zina nafasi ya pekee sana katika maendeleo ya mwanadamu, lakini pia zinachangia kwa kiasi kikubwa uharibu wa mazingira, jambo ambalo haliwezi kamwe kufumbiwa macho! Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa, UNEP linasema kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kutafuta mbinu mkakati utakaodhibiti uchafuzi wa mazingira unaosababishwa na taka za plastiki.

Umoja wa Mataifa unasema, kuna haja ya kupunguza matumizi yake, kuzitumia au kuzigeuza na kuwa bidhaa nyingine. Lengo ni kudhibiti uchafuzi wa mazingira unaofanywa na taka za plastiki, jambo linaloweza kuwa ni mzigo mkubwa katika ukuaji wa uchumi. Mkutano huu wa Umoja wa Mataifa kuhusu mazingira unahudhuriwa na wajumbe kutoka katika nchi 160 wanachama wa UNEP, kwenye Makao makuu ya UNEP, Nairobi, Kenya.







All the contents on this site are copyrighted ©.