Kila mwaka ifikapo tarehe 25 Juni, Jumuiya ya Kimataifa inaadhimisha Siku ya Mabaharia
Duniani. Hawa ni watu wanaofanya kazi kwa muda mrefu katika kipindi chote cha mwaka,
ili kuhakikisha kwamba, mizigo wanayoshughulikia bandarini inawafikia walengwa kwa
wakati muafaka. Hii ni sehemu ya ujumbe kutoka kwa Bwana Koji Sekimizu, wakati huu
wa maadhimisho wa Siku ya Mabaharia Duniani.
Kuna Meli
ambazo zimesheheni mizigo kutoka sehemu mbali mbali za dunia zinazohitaji kupakuliwa
kwa ajili ya walaji wa Ulaya. Ni mazao ya wakulima kutoka mashambani, madini na malighafi
kwa ajili ya matumizi ya viwanda. Hizi ni meli zinazobeba nishati ya mafuta na bidhaa
zake kwa ajili ya matumizi mbali mbali ya binadamu. Shughuli zote hizi zinazalisha
pato kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya mabillioni ya watu duniani.
Lakini
inasikitisha kuona kwamba, Mabaharia wapatao millioni 1. 5 wanakabiliwa na hali ngumu
ya maisha kila siku, lakini hawa ndio injini ya uzalishaji na ukuaji wa uchumi kimataifa.
Ni watu wanaoishi na kukabiliana na hatari kwa kufanya kazi katika mazingira magumu
na hatarishi, katika hali mbali mbali za hewa, ni kundi ambalo linapata fursa kiduchu
ya kukutana na kuchanganyikana na watu wengine katika Jamii. Kazi ni ngumu inayohitaji
uwajibikaji makini.
Mabaharia wanajikuta kwamba, kwa muda mrefu wanatengana
na familia zao; wanatishiwa maisha kutokana na vitendo vya kiharamia vinavyofanywa
huko Baharini. Siku ya Mabaharia Duniani ni mwaliko kwa wananchi sehemu mbali mbali
za dunia kuonesha mshikamano na Mabaharia pamoja na kuwapongeza kwa kazi kubwa wanayoifanya
kwa ajili ya kusukuma mbele gurudumu la maendeleo na uchumi wa dunia.
Bwana
Koji Sekimizu anasema, Maadhimisho ya Siku ya Mabaharia kwa Mwaka 2013 yalipata mafanikio
makubwa kwani vyombo vingi vya mawasiliano ya jamii, vilishiriki katika kuunga mkono
kampeni ya maadhimisho ya siku hii. Hata mwaka huu, watu wanahamasishwa kushiriki
katika kampeni ya kuunga mkono juhudi za maboresho ya maisha ya Mabaharia sehemu mbali
mbali za dunia. Hawa ni watu ambao wamewaonjesha mamillioni ya watu huduma mbali mbali
kwa njia ya bidhaa zinazotumika, kumbe kuna haja ya kusema, asanteni Mabaharia.