Askofu mkuu Dieudonne Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui, Jamhuri ya Watu wa Afrika
ya Kati anasema, Kanisa halina budi kuwa mstari wa mbele katika kukuza na kuendeleza
majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam nchini humo, ili kudumisha misingi
ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa kwa kutambua kwamba, wote ni watoto
wa Mwenyezi Mungu na tofauti zao za kiimani zisiwe ni chanzo cha vita na vurugu, bali
baraka na neema ya kusaidiana kama ndugu!
Inasikitisha
kuona kwamba, zaidi ya waamini wa dini ya Kiislam mia sita walilazimika kuyakimbia
makazi yao kutokana na machafuko ya kijamii yanayoendelea nchini humo. Askofu mkuu
Nzapalainga kwa kuonesha mshikamano wa upendo na udugu, alikwenda kuwatembelea na
kuwapatia msaada waliokuwa wanauhitaji katika kipindi hiki kigumu cha historia ya
nchi yao.
Kwa upande mwingine inafurahisha kuona kwamba, viongozi wa kidini
kwa pamoja waliwatembelea waamini hao na kuwafariji. Kuna baadhi ya viongozi wa dini
ya Kiislam waliopewa hifadhi kwenye makazi ya Askofu mkuu Nzapalainga katika kipindi
cha miezi mitano.
Anasema, kuna umuhimu kwa waamini na watu wenye mapenzi
mema kujifunza kuishi kwa umoja na mapendo pasi na kutawaliwa na chuki ambazo hazina
mashiko kwa maendeleo na ustawi wa watu. Kwa hakika majadiliano ya kidini yanafanyika
kwa njia ya ushuhuda wa maisha katika uhalisia wake.