2014-06-23 08:27:18

Wananchi wanalilia amani na utulivu!


Askofu mkuu Dieudonne Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati anasema, Kanisa halina budi kuwa mstari wa mbele katika kukuza na kuendeleza majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam nchini humo, ili kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa kwa kutambua kwamba, wote ni watoto wa Mwenyezi Mungu na tofauti zao za kiimani zisiwe ni chanzo cha vita na vurugu, bali baraka na neema ya kusaidiana kama ndugu! RealAudioMP3

Inasikitisha kuona kwamba, zaidi ya waamini wa dini ya Kiislam mia sita walilazimika kuyakimbia makazi yao kutokana na machafuko ya kijamii yanayoendelea nchini humo. Askofu mkuu Nzapalainga kwa kuonesha mshikamano wa upendo na udugu, alikwenda kuwatembelea na kuwapatia msaada waliokuwa wanauhitaji katika kipindi hiki kigumu cha historia ya nchi yao.

Kwa upande mwingine inafurahisha kuona kwamba, viongozi wa kidini kwa pamoja waliwatembelea waamini hao na kuwafariji. Kuna baadhi ya viongozi wa dini ya Kiislam waliopewa hifadhi kwenye makazi ya Askofu mkuu Nzapalainga katika kipindi cha miezi mitano.

Anasema, kuna umuhimu kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kujifunza kuishi kwa umoja na mapendo pasi na kutawaliwa na chuki ambazo hazina mashiko kwa maendeleo na ustawi wa watu. Kwa hakika majadiliano ya kidini yanafanyika kwa njia ya ushuhuda wa maisha katika uhalisia wake.








All the contents on this site are copyrighted ©.