Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi asubuhi, tarehe 21 Juni 2014 ameianza hija yake
ya kichungaji Jimboni Cassano allo Jonio, lililoko Calabria, Kusini kwa Italia, kwa
kuwatembelea na kuzungumza na wafungwa pamoja na askari magereza wa Castrovillari
ili kuonesha mshikamano wa Papa na Kanisa kwa wafungwa sehemu mbali mbali za dunia,
kama kielelezo cha utekelezaji wa matendo ya huruma, kadiri ya mafundisho ya Yesu
mwenyewe!
Baba Mtakatifu anasema, tafakari yake na wafungwa inagusia kwa namna
ya pekee haki msingi za binadamu na mahitaji msingi msingi ya wafungwa wanaotekeleza
adhabu yao wakiwa gerezani na kwamba, sera za huduma magerezani ni jambo linalopaswa
kupewa kipaumbele cha pekee kwa kusindikizwa na mikakati inayomwezesha mfungwa anapomaliza
kutumikia kifungo chake aweze kujiunga tena na Jamii. malengo haya yanaposhindwa kutekelezwa
matokeo yake ni adhabu zinazotolewa magerezani zinakuwa ni mzigo na uharibifu wa maisha
ya kijamii na kwa mhusika na jamii inayomzunguka.
Baba Mtakatifu anawakumbusha
wafungwa kwamba, mchakato unaopania kumrekebisha mfungwa ili anapomaliza adhabu yake
aweze kujiunga tena na Jamii si tu juhudi za kibinadamu bali pia hapa kuna haja kwa
wafungwa wenyewe kujibidisha kukutana na Mwenyezi Mungu ili kumwachia nafasi aweze
kuwafunda, kwani anawapenda, anawafahamu na ana uwezo wa kuwasamehe makosa yao. Yesu
ni mwalimu anayeweza kuwasaidia kujiunga tena na Jamii zao, kwa kuwashika mkono na
kuwarejesha tena kwenye Jamii. Mwenyezi Mungu daima anasamehe na kuongoza; anaelewa
na kungoja ili mwanadamu aweze kumwelewa, kusamahe na kuongozwa naye!
Ni matumaini
ya Baba Mtakatifu kwamba, muda huu wa kutumikia adhabu ya kifungo gerezani hautapotea
bure, bali utakuwa ni muda makini kabisa, kwa ajili ya kuomba na kupata neema kutoka
kwa Mwenyezi Mungu ya kubadilika na kuwa watu wema zaidi sanjari na mwelekeo mpya
wa kijamii kwani matendo mbali mbali yanayofanywa ndani ya jamii yanachangia katika
wema au ubaya wa Familia ya binadamu.
Baba Mtakatifu amewakumbuka na kuwaombea
wanafamia wote wa wafungwa walioko magerezani, ili Mwenyezi Mungu aweze kuwakirimia
utulivu na amani na kwamba, anapenda kuwatia shime askari magereza na wote wanaowahudumia
wafungwa kutekeleza dhamani hii kwa unyofu mkubwa.
Wakati huo huo Bwana Fedele
Rizzo, Mkuu wa Gereza la Castrovillari, kwa niaba ya askari magereza na wafanyakazi
wote wa Gereza hilo anapenda kumshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kuwatembelea,
kuwafariji na kuwatia moyo, tukio ambalo limeacha chapa ya kudumu katika akili na
mioyo yao. Wanampongeza kwa kuonesha mshikamano na watu, kiasi kwamba, watu wengi
wanapenda kumwona na kumsikiliza kutokana na ushuhuda wa maisha yake yanayojikita
katika unyofu, kiasi na uadilifu.
Naye Ivan, mmoja wa wafungwa wanaotumikia
kifungo Gerezani hapo kwa niaba ya wafungwa wenzake, amemshukuru Baba Mtakatifu kwa
kuwatembelea Kondoo waliopotea ili aweze kuwarudisha tena Zizini. Uwepo wake hapo
Gerezani ni kielelezo cha Mchungaji mwema anayejali na kuguswa na mahangaiko ya watu
wake.
Baba Mtakatifu anaonesha ile sura ya Mungu anayeendelea kumtafuta mwanadamu
aliyepotea ili aweze kumwonjesha upendo na huruma akiheshimu mchakato wa kila mfungwa
katika jitihada za kujirekebisha tena kutokana na mapungufu na makosa yake ya kibinadamu
yaliyopelekea hata akatiwa hatiani. Wafungwa hao wamemhakikishia Baba Mtakatifu kwamba,
wataendelea kumsindikiza kwa sala na kamwe hawatasahau siku hii aliyowatembelea na
kuwasalimia.