Ekaristi Takatifu ni Sherehe ya Kuabudu na Kushukuru!
Maadhimisho ya Sherehe ya Ekaristi Takatifu yanapania kumshangilia Yesu Kristo Mkate
ulioshuka kutoka mbinguni. Kanisa linamshukuru Yesu kwa zawadi kubwa ya Fumbo la Ekaristi
Takatifu lililoanzishwa na Yesu mwenyewe Siku ile iliyotangulia kuteswa kwake.
Hii
ni Sherehe inayoonesha moyo wa shukrani na ibada kuabudu Ekaristi Takatifu inayotembezwa
mitaani, kuonesha imani ya Wakristo wanaotembea na kumwabudu Yesu; mambo msingi katika
Sherehe ya Ekaristi Taktifu. Wakristo watambue kwamba, wao ni watu wanaojipambanua
kwa kumwabudu Mwenyezi Mungu, chemchemi ya upendo iliyofunuliwa kwao kwa njia ya Yesu
Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Upendo wa Yesu unaendelea
kujionesha ndani ya Kanisa.
Waamini wanaonesha imani yao kwa Fumbo la Ekaristi
Takatifu, kwa kumkataa Shetani na mambo yake yote, kwa kuyatakaa malimwengu na fahari
zake zinazojionesha katika uchu wa mali na madaraka; mambo yanayomjengea mwanadamu
kiburi! Waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee kumwabudu Yesu peke yake, anayeonesha
uwamo wake endelevu katika Fumbo la Ekaristi Takatifu, mwaliko kwa waamini kutambua
imani wanayoiungama katika Fumbo la Ekaristi Takatifu. Waamini wamwombe Kristo ili
awapatie mwanga na neema ya toba na wongofu wa ndani, ili kweli waamini waweze kumwabudu
Yesu Peke yake na wala si vinginevyo!
Ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na
Baba Mtakatifu Francisko wakati wa maadhimisho ya Ibada ya Misa takatifu, Sherehe
ya Ekaristi Takatifu kwenye Jimbo Katoliki la Cassano allo Jonio, Calabria, Kusini
mwa Italia, Jumamosi jioni, tarehe 21 Juni 2014. Kanisa linaungama imani kwa Yesu
Kristo: Mungu kweli na Mtu kweli; ambaye yumo katika maumbo ya mkate na divai, anayewachangamotisha
waamini kujibidisha kufanya hija pamoja naye, huku wakitekeleza ile amri kuu ya upendo
kwa Mungu na jirani. Watambue kwamba, wao ni watu wanaomwambudu Mungu katika Fumbo
la Ekaristi Takatifu, watu wanaofanya hija katika upendo.
Baba Mtakatifu anasema,
yuko kati yao ili kuwaimarisha katika msingi wa imani na mapendo pamoja na kuendelea
kuwatia shime katika hija wanayoifanya pamoja na Yesu chemchemi ya upendo. Baba Mtakatifu
anawashukuru na kuwapongeza Makleri wanaotekeleza utume wao Jimboni Cassano na Calabria
katika ujumla wake. Makleri hawa wanaendelea kujisadaka kwa ujasiri katika utekelezaji
wa mchakato wa Uinjilishaji mpya, kwa njia ya mtindo wa maisha unaotoa kipaumbele
cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Baba Mtakatifu
anawashukuru viongozi wa Kisiasa na Serikali wanaotekeleza wajibu wao kwa kuzingatia
kwanza kabisa mafao ya wengi, kwa kutambua kwamba, uongozi ni huduma. Anawataka waamini
na wananchi wote wenye mapenzi mema, kutolea ushuhuda unaojikita katika maisha ya
watu, kwa kukazia haki, matumaini na huruma. Baba Mtakatifu anawashukuru waamini na
familia zao kwa kuonesha alama za matumaini zinazobubujika kutoka ndani ya familia
zao, parokia na vyama vya kitume. Yesu katika hija na wafuasi wake ataendelea kuamsha
ndani mwao alama za matumaini kwa vijana ili wawese kujisadaka kwa ajili yao na jirani
zao.
Baba Mtakatifu Francisko kwa mara nyingine tena anawataka vijana kutokubali
kupokonywa matumaini waliyo nayo! Waendelee kumwabudu na kuungana na Yesu Kristo na
kwa njia hii, wataweza kupingana na dhambi, ukosefu wa haki, matumizi ya nguvu, kwa
kujikita katika kutafuta kilicho chema, kizuri na kweli.
Fumbo la Ekaristi
Takatifu ni kifungo cha umoja na upendo, kinachowaunganisha waamini kuwa kweli ni
Familia moja; Watu wa Mungu wanaoungana kumzunguka Yesu, Mkate wa uzima wa milele.
Kwa kufanya hija na Yesu, Kanisa la Kijimbo na Parokia zitaweza kukua na kushamiri
katika imani, upendo na furaha katika mchakato wa Uinjilishaji. Hili litakuwa ni Kanisa
linalojengeka katika mshikamano wa upendo miongoni mwa watu wake, kwa kusaidiana na
kupendana kama ndugu, hasa nyakati za magumu na mahangaiko ya ndani.
wakati
huo huo, Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia
amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kutekeleza ahadi ya kuwatembelea, ili kukutana
na Kanisa ambalo linajipambanua kwa utume na ukarimu; watu wanaotaka kufanya mabadiliko
katika maisha yao, ili kujijengea uwezo wa kiuchumi pamoja na kupambana na vitendo
vinavyodhalilisha utu na heshima ya binadamu kama vile "Ndragheta". Majiundo makini
yanayotolewa kwa waamini yanapania kuamsha tena dhamiri nyofu, ili kutangaza na kuishuhudia
Injili ya Furaha.
Anamshukuru Baba Mtakatifu kwa kuomba msamaha, lakini Askofu
Galantino kwa upande wake anaomba pia msamaha kwa kutowaonjesha watu wake huruma na
msamaha. Anawakumbatia Makleri, Watawa na wagonjwa wote wa Jimbo lake.