Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kufanya hija ya kichungaji Jimboni Cassano all’Jonio
liliko Kusini mwa Italia hapo tarehe 21 Juni 2014, wakati wa maandalizi ya Siku kuu
ya Ekaristi Takatifu.
Askofu Nunzio
Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia anasema kwamba, Baba
Mtakatifu atapata fursa ya kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu majira ya jioni saa
11:00 kwa saa za Ulaya.
Waamini wanatambua zawadi kubwa ambayo Baba Mtakatifu
anatarajia kuwapatia kwa kuwatembelea ili kuwaimarisha katika imani, matumaini na
mapendo, ili wao pia waweze kuwa kweli ni Ekaristi kwa ajili ya jirani zao, hasa wakati
huu Mama Kanisa anapojikita katika mchakato wa Uinjilishaji mpya, unaodai ushuhuda
wa imani kwa Kristo na Kanisa lake!
Jimbo hili linaundwa na Jumuiya ndogo
ya waamini, ni eneo ambalo linaweza kusahauliwa ki-urahisi, lakini imeonekana kuwa
na thamani kubwa machoni pa Baba Mtakatifu Francisko, kiasi hata cha kumteuwa Askofu
wake Nunzio Galantino kuwa Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia. Baba
Mtakatifu alisema anapenda kuwatembelea ili kuwaomba waamini msamaha kwa kuwaondolea
Askofu Nunzio Galantino, kipenzi chao kwa kumpatia utume mwingine! Kumbe, maandalizi
ya hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko Jimboni Cassano All’Jonio inaongozwa
kwa kauli mbiu “Hata sisi tunaomba msamaha”.
Waamini wanapenda kumwomba Mwenyezi
Mungu msamaha kutoka katika undani wa mioyo yao kwa kuwaacha maskini na watu wanaosukumizwa
pembezoni peke yao katika shida na mahangaiko yao. Hapa waamini wanataka sasa kuwa
na mwamko mpya wa kujimega bila ya kujibakiza kwa ajili ya mafao na ustawi wa jirani
zao. Ni mwaliko wa kuwa kweli ni watu wa Kiekaristi.
Waamini wanaomba msamaha
kwa vijana kwa kutowasaidia kutimiza ndoto zao, sasa Jimbo linataka kutoa kipaumbele
cha pekee katika majiundo awali na endelevu kwa vijana ili waweze kuwa kuweli ni washiriki
wakuu katika Uinjilishaji Mpya. Kanisa linataka kuwajengea vijana na watoto uwezo
kwa njia ya elimu. Ni hija ya kuomba msamaha kwa wasio amini, ili kuanza mchakato
wa majadiliano, ili hatimaye, waweze kuonja utamu wa kukutana na Yesu Kristo mkombozi
wa ulimwengu.
Hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko jimboni humo
ni changamoto ya kuangalia mikakati ya kichungaji kadiri ya vipaumbele vinavyoendelea
kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wa Kanisa kwa nyakati
hizi: ushuhuda wa imani kwa Kristo na Kanisa lake, utu na heshima ya binadamu, mshikamano
na upendo kwa kukazia mambo msingi katika maisha. Ni fursa ya kuondokana na ubinafsi.
Hija ya Baba Mtakatifu ni changamoto makini kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu.