Kumbu kumbu ya Mtaguso wa NICEA kufanyika mwaka 2025
Hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilee
ya miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana na kusali pamoja na Patriaki Anathegoras
wa Yerusalem, limekuwa ni tukio ambalo limeamsha tena hisia za kuendeleza majadiliano
ya kiekumene kati yake na Patriki Bartolomeo wa kwanza wa Costantinopoli.
Viongozi hawa
wawili wanaendeleza mchakato wa majadiliano ya kiekumene ili kuponya madonda ya utengano
miongoni mwa Wakristo. Panapo majaliwa, viongozi hawa wamepanga tena kukutana na kusali
pamoja kunako mwaka 2025, kama kumbu kumbu ya Mtaguso wa Nicea uliofanyika kunako
mwaka 325, yapata karne kumi na saba zilizopita. Hii ilikuwa ni Sinodi ya kiekumene
iliyoandika Kanuni ya Imani anasema Patriaki Bartolomeo wa kwanza wakati akizungumza
na Shirika la Habari la Asia News.
Mtaguso wa Nicea uliofanyika kunako mwaka
325 uliwakusanya Maaskofu 300 kutoka Makanisa ya Mashariki na Magharibi na hapo wakaandika
Kanuni ya Imani inayoendelea kutumika hadi leo hii katika Ibadan a Liturujia mbali
mbali za Kanisa. Hii ni mipango ya muda mrefu ili kuganga na kuponya madonda ya utengano
miongoni mwa Wakristo. Kwa wakati huu viongozi hawa wawili wanaendelea kujielekeza
zaidi na zaidi katika kuimarisha na kukuza urafiki na ushirikiano wa kiekumene baina
ya Makanisa haya mawili.
Akizungumzia kuhusu mkutano huu, Professa R. Andrew
Chesnut kutoka Chuo Kikuu cha Commonweath anasema, tukio hili si tu kwa ajili ya kuendelea
kuboresha mahusiano ya kiekumene baina ya Makanisa haya mawili, bali pia unalenga
zaidi kuunga mkono Wakristo wanaoishi huko Mashariki ya kati.
Viongozi hawa
wawili wamekuwa mstari wa mbele kwa ajili ya kuwatetea Wakristo wanaoteseka na kudhulumiwa
huko Mashariki ya Kati na kwamba, idadi ya waamini wa Makanisa haya inaendelea kupungua
mwaka hadi mwaka kutokana na madhulumu ya kidini.