Mpendwa mwana wa Mungu, ninakuletea Tafakari ya Liturujia ya Neno la Mungu leo ikiwa
ni Sherehe ya Mwili na Damu ya Bwana wetu Yesu Kristu. Sherehe hii ni kati ya sherehe
za Bwana na huadhimishwa Dominika inayofuata mara baada ya sherehe ya Utatu Mtakatifu.
Ni sherehe
ambayo ina uhusiano wa moja kwa moja na Alhamisi kuu ambapo Fumbo la Ekaristi Takatifu
linawekwa katika Kanisa na Yesu Kristu mwenyewe. Siku ya Alhamis Kuu hatukupata nafasi
ya kusherehekea hasa kwa shangwe na nderemo kwa kuwa tulikuwa tayari katika Juma Kuu,
Juma la Mateso ya Bwana. Kumbe, Mama Kanisa anatujalia nafasi tena ya kusherehekea
na kushangilia kwa vigelegele sherehe hii hivi leo.
Ndiyo kusema katika sikukuu
hii tunafanya ukumbusho wa Karamu ya mwisho, ambapo Bwana alikula karamu hiyo pamoja
na wanafunzi wake. Ni katika karamu hiyo aliweka sakramenti ya Ekaristi na sakramenti
ya Upadre. Mama Kanisa hufanya maandamano katika siku hii ikiwa ni ishara ya ushuhuda
wa imani akitangaza ukuu wa Mungu kwa mataifa ambao hujidhihirisha kwa njia ya Ekaristi
Takatifu. Ni ishara ya shukrani kwa Mungu kwa ajili ya zawadi ya Mwili na Damu ya
Bwana wetu Yesu Kristu. Ekaristi Takatifu ni chimbuko la Kanisa na hivi tunasherehekea
na kushangilia zawadi ya Kanisa kama Safina ya wokovu.
Mpendwa mwana wa Mungu,
tunaposherehekea Sherehe ya Mwili na Damu ya Bwana kwa shangwe Mama Kanisa atuwekea
Neno la Bwana akitaka polepole kutambua hicho tunachokisherehekea kuwa ni kitu cha
thamani kuu. Bwana anasema “twaeni mle na mnywe wote huu ndio mwili na hii ndiyo Damu
yangu itakayomwagika kwa ajili ya wengi”. Mwinjili Yohane akikazia na kuleta maana
ya maneno haya anamnukuu Bwana akisema “mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka
kutoka mbinguni, mtu akila chakula hiki ataishi milele”.
Mpendwa msikilizaji,
maneno haya tunayapata katika sura ya 6 ya Injili ya Yohane ambayo ni mahubiri juu
ya mkate wa uzima. Katika sura hiyo ya 6 Bwana anaanza na mwujiza wa ongezeko la mikate
na samaki ambapo aliwalisha watu 5000 wanaume tu, kumbuka wanawake na watoto hawakuhesabiwa,
kumbe walikuwa zaidi!
Walipokwishamaliza kula walikusanya mabaki vikapu 12
na neno juu ya hili: hakika huyu ndiye Nabii anayekuja ulimwenguni. Muujiza huu ulionesha
upendo wake kwa watu na kwa namna hii alitangaza kuwa ataweka kitu kingine zaidi ya
hicho anapomalizia kazi yake ya kitume hapa duniani. Kukusanya vikapu 12 mabaki, tayari
kunaashiria kutoisha kwa Ekaristi Takatifu atakayoiweka baadaye.
Hawa watu
aliowalisha kwa mikate na samaki baadaye walitaka kumfanya awe mfalme na hapa ndipo
anagundua ufinyu wa mawazo na mwono wao na hivi anataka wasonge mbele toka hatua hiyo
na kukifanyia kazi chakula kisichoharibika yaani chakula cha uzima wa milele-ndiyo
Ekaristi Takatifu Mwili na Damu yake.
Katika majadiliano, Bwana alipokwisha
kuwaambia chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu kwa ajili ya uzima wa ulimwengu,
wanauliza hivi awezaje kutupa mwili wake mtu huyu tuule? Ni kweli maneno ya Bwana
ni magumu kama yale aliyomwambia mwanamke msamaria yaani yakumpa maji ya uhai na mwanamke
anashangaa! (Yn 4:14-15).
Kwetu sisi leo maneno kama mkate wa mbinguni ni
rahisi kuyaelewa yaani Neno la Mungu ambalo hujifungamanisha na maisha yetu katika
Yesu Kristu mwenyewe. Ndiyo kusema Yesu ndiye mkate wa uzima. Tunampokea Bwana na
anakuwa maisha yetu na hivi tunazaliwa upya katika upendo kwa wengine na hii ndiyo
maana ya Ekaristi Takatifu.
Bwana anasonga mbele katika mahubiri yake akisema
aulaye mwili wangu na kuinywa Damu yangu anao uzima wa milele na atafufuliwa siku
ya mwisho. Kama vile yeye ambavyo alikufa na kufufuka basi aulaye mwili wake anajiunganisha
na yeye na kujipatia asili ya Bwana, anajitoa yeye mwenyewe kwa ajili ya Bwana ili
aweze kuendelea kuteseka, kujitoa na hatimaye kufufuka katikati ya maisha yetu.
Katika
hili tunamwona Mtakatifu Paulo akisistiza kwamba kabla ya kula mkate huu mtakatifu
lazima kujichunguza kwanza ili kuona kama anastahili kweli na hivi kuweza kuruhusu
Kristu aendelee kuishi ndani mwake na katika jumuiya (1Kor 11:28) Katika hili lazima
kutambua kuwa kabla ya Ekaristi lazima kujiandaa kiimani, kama kweli tunataka kugeuzwa
na kuwa Kristu mwingine.
Katika hali ya kawaida mkristu hapokei Ekaristi bila
kusikia Neno la Mungu, ambalo kwanza huangaza maisha yake na humfanya aingie katika
ulimwengu wa Kristu, ndiyo kusema lazima kwanza agundue nani ni Kristu, anasema nini,
anafundisha nini na akisha kumpokea Kristu anataka nini baadaye katika maisha ya watu
na jumuiya kwa ujumla. Bila hili ni vema tukasubiri kwanza kabla ya kuanza kuandamana.
Katika
Fumbo la Ekaristi, ipo hatua nyingine muhimu kadiri ya utamaduni wa kanisa tangu zamani.
Hatua hii ni ile ya kumwabudu Bwana, ni hali ya kukaa mbele ya Ekaristi Takatifu Kristo
mwenyewe na kumweleza hali yako, kumsifu na kumtukuza ukichota nguvu kwa ajili ya
maisha ya pamoja katika jumuiya. Mmoja huenda pale mbele ya Bwana aliyeupendo vunjika
ili apate naye kuwa kipande cha upendo kwa wengine. Hali ya kuabudu na kusifu huwa
yenye kuzaa matunda kama tunashiriki Misa Takatifu yaani maadhimisho ya kijumuiya,
ndiyo maana katika sherehe hii huanza Misa na baadaye kusifu na kuabudu.
Mpendwa
msikilizaji, tunapopokea Mwili na Damu ya Bwana, tunapokea mwanga katika maisha yetu
maana alisema mimi ni taa ya maisha yako, ni ukweli na uzima kumbe pia twahuishwa
na Bwana anayetaka toka maisha hayo tukafanye vivyo hivyo daima mpaka ajapo. Anatualika
kwa njia ya Ekaristi tuishi uhuru wa wana wa Mungu aliotupatia Bwana (Lk. 4:18 na
kuendelea).Tunaalikwa kukumbuka Wana wa Israeli walipopatwa na taabu jangwani, ilikuwa
ni “neno la Mungu” lililowaletea manna hukohuko jangwani.
Chakula hiki kilikuwa
ni chakula kipya kabisa. Ndiyo kusema mwandishi ataka kusema kuwa Neno la Mungu ni
nguvu na nyenzo ya kutatua matatizo mbalimbali katika maisha yetu, hata kama tutakuwa
tumekata tamaa. Hali hii ndiyo ambayo tunaipata katika sehemu ya Injili ya leo.
Mpendwa
msikilizaji, Mtakatifu Paulo anapowaandikia Wakorinto anakuja na Ekaristi Takatifu
kama chimbuko na ndilo chimbuko la umoja. Anakemea utengano uliopo kwa sababu ya fikra
tofauti maana wengine walikuwa wamebaki na mawazo ya kipagani. Anasema “Je, Kikombe
kimoja tukibarikicho si ushirika wa Damu ya Kristu? Mkate tuumegao Je! Sasa ya nini
kuhukumiana na ufukuzana katika jumuiya? Je, inawezekanaje katika vurugu kama hizo
tukaketi na kunywea kikombe kimoja?
Basi Mtakatifu Paulo anakemea hilo katika
jumuiya Wakorinto na jumuiya yako hivi leo. Yafaa kwa hakika katika adhimisho hili
la sherehe ya Mwili na Damu kujifunza mapendo na huruma, msamaha na upole ili Kristu
aishi ndani mwetu nasi tuishi ndani mwake.
Mpendwa msikilizaji, tunaposherehekea
tunapaswa kufikiri kwa undani sana nini maana ya fumbo hili kuu na mwisho lazima,
tafakari yetu imalizikie katika neno moja “PENDANENI KAMA NILIVYOWAPENDA NINYI”. Ninakutakieni
furaha tele nikikukumbusha maneno ya Bwana “fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu hadi
nitakaporudi”. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard
Tiganya C.PP.S.