Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 20 Juni 2014 amekutana na wajumbe waliokuwa
wanashiriki kwenye mkutano wa kimataifa kuhusu uthibiti wa dawa za kulevya, tatizo
ambalo linaendelea kusababisha majanga makubwa kwa watu wa nyakati hizi.
Ni
matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, mkutano wao utazaa matunda yanayokusudiwa lakini
zaidi kwa kufikia malengo waliyojiwekea wakati wa mkutano huu uliokuwa unafanyika
mjini Roma yaani: kuratibu sera za kupambana na matumizi haramu ya dawa za kulevya,
kushirikishana habari pamoja na kuibua mbinu mkakati utakaotumika kwa ajili ya kudhibiti
biashara haramu ya dawa za kulevya.
Baba Mtakatifu anasema biashara haramu
ya dawa za kulevya ni janga ambalo linaendelea kukua na kukomaa siku hadi siku, kiasi
cha kuvuka mipaka na jiografia za kitaifa hadi kufikia ngazi ya kimataifa, kiasi cha
kuhatarisha maisha ya vijana. Kutokana na hali hii, Baba Mtakatifu anasema anapenda
kuonesha wasi wasi na masikitiko yake makuu.
Jamii haiwezi kushinda vita dhidi
ya matumizi haramu ya dawa za kulevya kwa kuruhusu matumizi ya dawa hizi; wala kuponya
magonjwa kwa dawa za kulevya. Hapa kuna haja ya kusema wazi kwamba, hakuna sababu
ya msingi ya kuruhusu matumizi haramu ya dawa za kulevya, kwa kuonesha upendo kwa
zawadi ya uhai pamoja na kuwashirikisha wengine upendo.
Ni changamoto ya kujikita
katika kuwafunda vijana madhara ya matumizi haramu ya dawa za kulevya; kutengeneza
fursa za ajira pamoja na kuwekeza katika uzalishaji ili watu waweze kupata ajira.
Hakuna nafasi kwa matumizi haramu ya dawa za kulevya, ulevi wa kupindukia na wala
kuunda utegemezi kwa mambo mengine yanayodhalilisha utu na heshima ya binadamu!
Baba
Mtakatifu anasema Kanisa litaendelea kutekeleza dhamana na wajibu wake wa kuwahudumia
watu katika mahangaiko yao ya ndani, kwa kuwatibu wagonjwa, kuwalisha wenye njaa na
kuwatembelea wafungwa. Kanisa halitawaacha pweke wale waliotumbukia katika matumizi
haramu ya dawa za kulevya, atawasaidia ili waweze kutambua tena utu na heshima yao,
kwa kugundua rasilimali na karama zilizokuwa zimefunikwa na matumizi haramu ya dawa
za kulevya, kwani kila mtu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Vijana waliochakachua
maisha yao kwa kubwia dawa za kulevya, waanze mchakato wa kuboresha tena maisha yao,
kwa kuwa na matumaini kwa kesho iliyo bora zaidi.