2014-06-19 10:03:04

Msiuze kura zenu mtafilisika kidemokrasia!


Askofu Benjamin Ndiaye, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu kutoka Senegal, Mauritania, Cape Verde na Guinea Bissau amewataka wananchi wa Senegal kutouza kura zao kwa wanasiasa walaghai wanaotaka kujinufaisha wao wenyewe, bali wahakikishe kwamba, wanatumia kura yao vyema kama sehemu ya mchakato wa kushiriki katika ujenzi wa nchi yao. Kila mtu achague kiongozi anayemtaka kwa kufuata dhamiri yake nyofu na kamwe wasikubali kununulia kwama bidhaa sokoni na hivyo kupoteza uhuru wao kidemokrasia!

Askofu Ndiaye anawataka pia wanasiasa wanaojiandaa kushiriki kwenye kinyang'anyiro cha madaraka wakati wa uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini Senegal Jumapili tarehe 29 Juni 2014 kudumisha misingi ya haki, amani na mshikamano wa kitaifa; daima walenge kusimamia kidete mafao ya wengi, ili hatimaye, waweze kuleta mabadiliko makubwa yanayotarajiwa na wananchi wengi wa Senegal.

Halmashauri ya Walei Jimbo kuu la Dakar, Senegal linawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kushiriki kwa kikamilifu pamoja na kuhakikisha kwamba, uchaguzi unaendeshwa kwa misingi ya ukweli, uhuru na haki. Uchaguzi mkuu uliopita nchini Senegal, uliacha kurasa chungu na za majonzi kwa wananchi wengi, jambo hili lisijirudie tena, kwa viongozi wa kisiasa na mashabiki wao kuendesha kampeni za kitastaarabu, zinazoheshimu na kuzingatia utawala wa sheria, ushindani wa nguvu ya hoja na mikakati thabiti ya maendeleo ya watu. Lengo ni kuunda Serikali ambayo itajikita katika mchakato wa kuendeleza mafao ya wengi na maendeleo endelevu ya wananchi wa Senegal.







All the contents on this site are copyrighted ©.