2014-06-19 09:46:29

Msijenge chuki na visasi, Kenya itachafuka tena!


Askofu Emmanuel Barbara, wa Jimbo la Malindi na msimamizi wa kitume Jimbo kuu la Mombasa, Kenya amewataka waamini na wananchi wanaoishi kwenye Ukanda wa Pwani kuwa macho na watu wanaotaka kuchafua misingi ya haki, amani na utulivu kutokana na kukithiri kwa mashambulizi ya kigaidi ambayo yanaendelea kusababisha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia.

Vitendo vya kigaidi vinaendelea kusababisha hofu na maafa makubwa kwa wananchi wa Kenya. Mauaji ya watu kwa misingi ya kidini ni dhana chafu sana inayoweza kusababisha kinzani na migogoro ya kidini isiyokuwa na mashiko wala tija anasema Askofu Barbara wa Jimbo Katoliki la Malindi. Mashambulizi ya hivi karibuni yaliyofanywa kwenye kitongoji cha Mpeketoni yalikuwa yameandaliwa kwa ufundi mkubwa.

Kinzani na migogoro ya kisiasa kati ya Serikali na Vyama vya upinzani ni cheche ambazo zinaweza kupelekea ukosefu wa amani na utulivu nchini Kenya. Askofu Barbara anawataka wananchi wote wa Kenya kushinda kishawishi ya kugubikwa kwa chuki, uhasama na moyo wa kutaka kulipizana kisasi!







All the contents on this site are copyrighted ©.