2014-06-18 08:21:24

Njaa bado inatesa watu duniani!


Askofu mkuu Luigi Travaglino, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Mashirika ya Umoja wa Mataifa yenye makao makuu yake mjini Roma, hivi karibuni alishiriki katika mkutano wa thelathini na mbili wa Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO kwa ajili ya Ukanda Amerika ya Kusini na Caraibi kwa kusema kuna haja ya kutoa majibu makini kwa watu wanaoteseka kwa baa la njaa duniani. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu Francisko anasikitika kusema kwamba, hata katika ulimwengu wa maendeleo ya sayansi, teknolojia, uzalishaji na tija, bado kuna watu wanakufa kwa baa la njaa duniani wakati sehemu nyingine za dunia, watu wanaendelea kushiba na kusaza, jambo ambalo halikubaliki kamwe.

Kuna chakula cha kutosha kuweaza kuganga baa la njaa, shida ni mgawanyo wa chakula hiki, changamoto ya kutoa mwelekeo wa kiutu zaidi kuliko kung’angania tu mwelekeo wa teknolojia katika uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara. Jumuiya ya Kimataifa haina budi kujikita katika uhakika wa usalama wa chakula duniani, kwa kuzalisha chakula cha kutosha pamoja na kuboresha ugavi wake.

Juhudi hizi hazina budi kwenda sanjari na mapambano dhidi ya umaskini wa hali na kipato unaoendelea kuwaandama watu wengi duniani pamoja na kuendelea kuimarisha mafanikio yaliyopatikana katika Malengo ya Maendeleo ya Millenia kwa Mwaka 2015, katika mchakato wa kupunguza kwa kiasi kikubwa idadi ya watu wanaoteseka kutokana na baa la njaa na utapimlo mkali duniani.

Mikakati ya mapambano dhidi ya baa la njaa na umaskini, inakwamishwa kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi ambayo yameendelea kuwa ni chanzo kikuu cha maafa sehemu mbali mbali za dunia. Sera tenge katika masuala ya uzalishaji, ugavi na masoko zimepelekea baadhi ya watu kunyimwa fursa ya kuuza mazao yao kwenye soko la pamoja, hali ambayo inazilazimisha baadhi ya nchi kuendelea kuagiza chakula cha msaada kutoka nje ya nchi zao! Ukosefu wa fursa za ajira hasa miongoni mwa vijana ni jambo linalochangia kuongezeka kwa umaskini miongoni mwa Jamii.

Mbinu mkakati wa kuwa na uhakika wa usalama wa chakula hauna budi kulenga zaidi katika uzalishaji wa mazao ya chakula vijijini, kwa kuzingatia wingi na ubora pamoja na kuwajengea uwezo wakulima wadogo wadogo kwa njia ya vyama vya ushirika. Mwaka wa Kimataifa wa Wakulima Vijijini unaoadhimishwa na Jumuiya ya Kimataifa, uliopendekezwa na Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO, usaidie kuweka mikakati makini ya shughuli za kilimo vijijini, kwa ajili ya maendeleo endelevu ya binadamu.

Askofu mkuu Luigi Travaglino anasema kwamba, Familia za wakulima vijijini, zikijengewa uwezo, zinaweza kushiriki vyema zaidi katika kulinda na kutunza mazingira kwani kazi na familia ni kama chanda na pete katika kudumisha misingi ya upendo, umoja na udugu kati ya watu pamoja na kuwasaidia wanyonge. Mageuzi ya kilimo yanayozingatia maendeleo ya kweli ya binadamu ni jambo la msingi. Wananchi wahusishwe kikamilifu katika ulinzi na usimamizi wa mazingira, kwani mipango na mikakati ya maendeleo isiyotoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu na mahitaji yake haina tija wala mashiko kwa maendeleo ya watu!

Mapambano dhidi ya baa la njaa yataweza kupata mafanikio makubwa, ikiwa kama wakulima, serikali, mashirika ya kimataifa, vyama vya kiraia, vyama vya ushirika na wawekezaji binafsi katika sekta ya kilimo watashirikishwa kikamilifu, ili kujenga na kuimarisha uchumi jamii unaokidhi mahitaji ya watu! Ili kufanikisha azma hii kanuni maadili ya mshikamano inapaswa kutekelezwa. Hii ni kanuni inayopewa msukumo wa pekee na Kanisa katika Mafundisho yake Jamii.

Ujumbe wa Vatican katika mkutano huu wa Kanda ya Amerika ya Kusini na Caraibi, umeipongeza FAO kwa kuendelea kushirikiana na Serikali mbali mbali katika mchakato wa kupambana na baa la njaa duniani. Vatican itaendelea kushirikisha mchango wake katika masuala ya kimaadili ili kuwa na siasa na sera makini za maendeleo zinazotoa kipaumbele cha kwanza kwa haki msingi za binadamu, utu na maendeleo yake endelevu!

Imeandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.