Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM kwa kushirikiana
na Baraza la Maaskofu Katoliki Benin, hivi karibuni limehitimisha warsha ya siku tatu
kama sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu familia
itakayoadhimishwa kuanzia tarehe 5 hadi 19 Oktoba, 2014 mjini Vatican.
Warsha
hii imepembua pamoja na mambo mengine furaha, changamoto na matatizo yanayozikabili
familia za Kiafrika katika mchakato wa kutangaza Injili ya Familia mintarafu dhamana
ya Uinjilishaji Mpya. Wajumbe wamejiandaa kushirikisha mchango wa Kanisa la Afrika
wakati wa maadhimisho haya, kwa kuangalia changamoto zinazoendelea kujitokeza Barani
Afrika, lakini zaidi, Familia ya Mungu Barani Afrika inapenda kushirikisha tunu bora
za maisha ya ndoa na familia zinazofumbatwa katika mila na desturi njema za Kiafrika.
Waamini,
vyama vya kitume na watu wote wenye mapenzi mema wanaendelea kuhamasishwa kusimama
kidete kulinda, kutetea na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia katika
ulimwengu mamboleo ambao unaonekana kutaka kufifisha Injili ya Familia. Itakumbukwa
kwamba, Sinodi ni chombo maalum ambacho Baba Mtakatifu Francisko analitaka Kanisa
kwa pamoja kuchambua Injili ya Familia ili hatimaye, kuibua mbinu mkakati utakaotumiwa
na Kanisa katika kujibu changamoto za kichungaji zinazoendelea kujitokeza kwa wakati
huu.
Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia, itaadhimishwa katika
awamu kuu mbili: awamu ya kwanza ni Oktoba 2014 na awamu ya Pili itaadhimishwa hapo
mwaka 2015, lakini hili ni tukio moja linalopania kuliwezesha Kanisa kutembea kwa
pamoja kama Familia ya Mungu inayowajibika.