2014-06-17 11:09:15

Miradi ya maendeleo 125 kwa ajili ya Amerika ya Kusini imepitishwa!


Viongozi wakuu wa Mfuko wa Maendeleo ya Watu ambao uko chini ya usimamizi wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum, limehitimisha mkutano wake wa mwaka uliokuwa unafanyika mjini Vatican kwa kupitisha miradi 125 kwa ajili ya maendeleo ya wakulima Amerika ya Kusini, kwa gharama ya dolla za kimarekani millioni 1, 8000. 000.

Mkutano huu umefanyika mjini Vatican ili kupata ushauri wa shughuli za kichungaji kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko, wakati huu Mama Kanisa anapojielekeza zaidi katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu na maendeleo yake kiroho na kimwili. Huu ni mfuko ambao kwa muda wa miaka ishirini na miwili umekuwa mstari wa mbele katika kuwajengea uwezo wenyeji, ili hatimaye, waweze kujitegemea na kujiendeleza wenyewe.

Miradi iliyopitishwa kwa mwaka huu inahusu hasa majiundo makini kwa watoto na vijana Amerika ya Kusini; uchimbaji wa visima vya maji safi na salama, makazi ya watu pamoja na huduma ya afya.

Baba Mtakatifu alipokuwa akizungumza na wajumbe wa Mfuko wa Maendeleo ya Watu alikazia umuhimu wa huduma inayotolewa na Mama Kanisa kwa ajili ya maendeleo ya watu na kwamba, hii ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya unaotekelezwa na Mama Kanisa kwa ajili ya mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kanisa halina budi kujielekeza katika mchakato wa kuwajengea vijana matumaini mapya kwa kuwapatia fursa za ajira pale inapowezekana, ili kukuza na kudumisha misingi ya maadili na utu wema, vinginevyo vijana hawa wanaweza kujikuta wakiwa ni wahanga wa vitendo vya kigaidi, mateja ya dawa za kulevya na biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo.

Wajumbe wamebadilishana mawazo na mang'amuzi yao kuhusu mikakati ya maendeleo, ushirikiano na utekelezaji wa miradi hii kwa ajili ya mafao na ustawi wa wananchi wa Amerika ya Kusini. Wajumbe wanasema umefika wakati kwa Mfuko wa Maendeleo ya watu kupanua wigo wake kijiografia, ili kukumbatia upendo na ukarimu unaooneshwa na Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Makanisa mahalia yanaendelea kuhamasishwa kushiriki na kuchangia katika mikakati ya maendeleo ya watu wao.







All the contents on this site are copyrighted ©.