Uinjilishaji kwa njia ya wongofu na ushuhuda wa imani ya Kikristo ndiyo kauli mbiu
itakayofanyiwa kazi wakati wa maadhimisho ya mkutano wa 18 wa Shirikisho la Mabaraza
ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na kati, AMECEA utakaofanyika, Lilongwe nchini
Malawi, kuanzia tarehe 16 – 26 Julai 2014. Mkutano huu ndio ulikuwa ni ajenda kuu
ya mkutano wa Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi uliohitimishwa hivi karibuni.
Hii itakuwa
ni mara ya tatu kwa Familia ya Mungu nchini Malawi kuwa mwenyeji wa maadhimisho ya
mkutano wa AMECEA. Kwa mara ya kwanza AMECEA ilifanya mkutano wake nchini Malawi kunako
mwaka 1979 kwa kujielekeza zaidi katika uanzishwaji na uimarishaji wa Jumuiya ndogo
ndogo za Kikristo kama sehemu ya utekelezaji wa mikakati ya shughuli za kichungaji
inayofanywana Maaskofu wa AMECEA. Kunako mwaka 1995 Malawi ikawa tena mwenyeji wa
maadhimisho ya mkutano mkuu wa 12 uliofanyika mjini Mangochi kwa kuangalia dhamana
ya Kanisa katika maendeleo mintarafu mwanga wa Sinodi ya Afrika.
Baraza la
Maaskofu Katoliki Malawi katika mkutano wake limejadili pia kuhusu hija yao ya kitume
inayofanyika kila baada ya miaka mitano mjini Vatican kwa kukutana, kusali na kuzungumza
na Baba Mtakatifu pamoja na viongozi waandamizi wa Mashirika ya Kipapa mjini Roma.
Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi, linatarajia kufanya hija yake ya kitume mjini
Vatican kuanzia 6 hadi tarehe 9 Novemba 2014 kadiri ya ratiba iliyotolewa na Sekretarieti
ya Vatican.
Maaskofu wamejadili pia kuhusu Chuo Kikuu cha Kikatoliki Malawi;
majiundo awali na endelevu ya Makasisi: Katiba ya Chama cha Wakarisimatiki Wakatoliki
nchini Malawi; hali ya kisiasa na kijamii wakati na baada ya uchaguzi mkuu nchini
humo. Maaskofu pia wamepokea taarifa ya kuhusu Misale ya Waamini kwa lugha ya Chichewa
pamoja na taarifa mbali mbali kutoka katika Sektretarieti ya Baraza la Maaskofu Katoliki
Malawi.