2014-06-17 09:36:23

Kanisa ni mama na mwalimu, linatumwa kuinjilisha!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu jioni tarehe 16 Juni 2014 amefungua Kongamano la shughuli za kichungaji Jimbo kuu la Roma kwa kuonesha umuhimu wa Waraka wa kichungaji uliotolewa na Mtumishi wa Mungu Paulo VI Evangelii Nuntiandi, Utangazaji wa Injili, kazi iliyohaririwa kwa ufundi mkubwa na Mtakatifu Yohane Paulo II.

Katika hija zake za kichungaji Jimboni Roma Baba Mtakatifu anasema amekutana na watu wenye imani thabiti na baadhi ya watu wamekata tamaa kutokana na ugumu wa maisha, kiasi hata cha kupoteza maana ya maisha, changamoto kwa Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, anawajengea waamini umuhimu wa kuthamini zawadi ya maisha kuanzia katika misingi ya kifamilia pamoja na kujitahidi kutenga nafasi kwa ajili ya kukaa na familia, ili kuonja upendo na uwepo wa wazazi ndani ya familia, ili watoto wasijisikie yatima hata kama wazazi wao bado wako hai!

Baba Mtakatifu anazitaka familia kuonesha moyo wa sadaka na shukrani kwa Mwenyezi Mungu kwa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Waamini watambue kwamba, mambo mengi waliyokirimiwa ni neema na zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, changamoto kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kujisadaka pia kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake.

Yesu amewahakikishia wafuasi wake kwamba, kamwe hatawaacha yatima, hivyo anawaalika kumsikiliza kwa makini na kuendelea kuwa na matumaini kwake, kwani kamwe hawezi kuwadanganya. Yesu amewafunuliwa wafuasi wake upendo unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu, mwaliko kwa waamini kupendana, kuthaminiana na kusaidiana katika hija ya maisha. Kuna idadi kubwa ya vijana ambao hawana fursa za ajira nchini Italia na Ulaya kwa ujumla, hawa ni watu wasiokuwa na nafasi, ni watu wanaopuuzwa na kutwezwa. Hii ndiyo taswira ya jamii ya kiteknolojia isiyojali wala kuguswa na mahangaiko ya wengine, jamii ambayo haina furaha hata kidogo.

Baba Mtakatifu anasema, kupenda na kuthamini zawadi ya maisha hakuna haja ya kuwa na mambo mengi, bali ni kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Yesu anayemkirimia mwamini mwelekeo mpya wa maisha unaojikita katika wongofu wa ndani, ari na mwelekeo wa kimissionari. Wongofu wa ndani ni hija inayohitaji ujasiri na kuona fadhila ya umama inayojikita katika maisha na utume wa Kanisa; wenye uwezo wa kuzaa watoto wapya kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo.

Yote haya ni matokeo ya mikakati ya shughuli za kichungaji zinazojielekeza katika Uinjilishaji Mpya. Kanisa halina budi kujisikia kuwa kweli ni Mama na Mwalimu kwa njia ya mtindo wa maisha na ushuhuda wenye mvuto na mashiko kama alivyowahi kusema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI. Kanisa halina budi kujipyaisha kwa kukazia maisha ya kifamilia na kijumuiya, mahali ambapo waamini wanakutana na kushirikishana kweli za Kiinjili; mahali ambapo kweli watu wanajisikia kuwa ni sehemu ya Familia ya Mungu.

Watu wajifunze kujisadaka kwa kutenga muda kwa ajili ya maisha na utume wa Kanisa. Kanisa lioneshe moyo wa upendo kwa njia ya ukarimu kwa wote wanaobisha hodi katika malango yake, hasa zaidi kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Baba Mtakatifu Francisko anawataka waamini kujenga na kudumisha moyo na utamaduni utakaowawezesha watu kujisikia kweli wako nyumbani wanapokuwa Kanisani. Anatambua dhamana na majukumu waliyo nayo Makleri katika utume na kazi za Uinjilishaji. Kashfa na makwazo yaliyotendwa na baadhi ya Makleri yamekuwa ni chanzo cha baadhi ya watu kutoonekana tena Kanisani, changamoto ya kujirekebisha na kuanza kweli kutoa ushuhuda wenye matumaini kwa Kanisa la Kristo.

Watu waonje huruma na upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo kwa njia ya Kanisa lake. Kanisa litafakari, fursa, matatizo na changamoto za vijana, ili liweze kuwasaidia kukua na kukomaa, ili kweli waweze kuwa ni watu wa matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi. Kanisa liwaonjeshe watu huruma ya Kristo, kwa njia ya ushuhuda wa maisha ya kila mwamini na wala si kutoka kwa Mapadre, Watawa na Makatekista au viongozi wa Halmashauri ya waamini walei peke yao.

Ratiba ya shughuli za kichungaji Parokiani iwawezeshe hata vijana kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Kanisa litumie fursa kama vile michezo na teknolojia mpya za mawasiliano ya jamii kuwashirikisha na kuwaonjesha vijana kweli za kiimani.

Baba Mtakatifu anawataka waamini wa Jimbo kuu la Roma kufanya upembuzi yakinifu katika mambo yanayopelekea watu wengi kujikuta wakiwa wamebaki kama watoto yatima; kugundua tena na kuimarisha tunu bora za maisha ya kifamilia pamoja na kukazia umuhimu wa Parokia kama Jumuiya ya Ukarimu. Makleri waendelee kujisadaka katika maisha na utume wao wa Kikuhani kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Mapadre wawe wapesi kusikiliza na kutoa huduma kwa wazee, wagonjwa pamoja na kushiriki katika misiba ya wanaparokia wao. Wajitahidi kuhakikisha kwamba, hakuna mtu anayefariki Parokiani kwao bila kupata huduma ya maisha ya kiroho pale inapowezekana! Kwa njia hii, Kanisa linaweza kutoka kifua mbele kwa ajili ya Uinjilishaji. Mwishoni, Baba Mtakatifu amewashukuru waamini wote waliohudhuria kwa uvumilivu na upendo wao na amewataka kuendelea kumwombea katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.







All the contents on this site are copyrighted ©.