2014-06-16 09:37:18

Zingatieni sala, huduma kwa maskini na amani!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili jioni tarehe 15 Juni 2014 ametembelea Jumuiya ya Mtakatifu Egidio na kukutana pamoja na kusali na maskini, wazee, wakimbizi na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii mjini Roma. Ameishukuru Jumuiya ya Mtakatifu Egidio kwa kukuza na kudumisha moyo wa sala, kama kielelezo cha ujenzi wa utamaduni wa kusikiliza na kuonesha ukarimu kwa wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Neno la Mungu ni huduma ya kwanza inayotolewa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio na hivyo kuwawezesha kuchota nguvu inayobubujika kutoka katika adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu, tayari kusonga mbele kwa imani na matumaini makubwa. Maskini hata katika umaskini wao wanaweza kusaidiana na hivyo kuunda Jumuiya inayojipambanua kwa kuwasaidia maskini, wazee na watoto, kielelezo makini cha Jamii inayojali na kuwajibika.

Wazee wanapokumbana na upweke hasi wanakata tamaa na hiki ni kielelezo hasi cha Jamii, changamoto kwa vijana na wazee kuchangamana na kusaidiana kwa kutambua kwamba, sala zao ni zawadi kubwa kwa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio. Jamii isiyotunza wazee na vijana, haina matumaini kwa siku za usoni. Sera na mikakati ya uchumi na maendeleo haina budi kutoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu na mahitaji yake msingi. Inasikitisha kuona kwamba, kuna idadi kubwa ya vijana wasiokuwa na fursa ya ajira na Barani Ulaya, mwaliko wa kulisaidia Bara hili kurudia tena mizizi ya maisha yake!

Maskini wakiwezeshwa wanaweza kufanya maajabu katika ustawi na maendeleo ya kijamii, lakini mikakati na uchumi wa maendeleo katika ulimwengu wa utandawazi unaendelea kuwatenga na kuwatumbukiza maskini katika baa la umaskini wa hali na kipato, kwa kukosa fursa za ajira na makazi bora na salama na matokeo yake, kuna umati mkubwa wa watu wanaotengatanga barabarani kutafuta riziki ya maisha. Mshikamano wa kidugu, ni matusi kwa baadhi ya watu! Jumuiya ya Mtakatifu Egidio ni kielelezo cha mshikamano wa upendo na watu wasiokuwa na makazi, wazee na wakimbizi wanaotafuta maisha bora ugenini.

Baba Mtakatifu anasema wakimbizi ni watu wanaotoka katika maeneo ya vita na majanga asilia; ni watu wanaotafuta amani na usalama wa maisha yao, mwaliko kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kuwa kweli ni vyombo vya ujenzi wa misingi ya haki, amani na utulivu, kwa kujikita katika sala na majadiliano zaidi, kwa watu kutambua na kuthamini utambulisho wao pamoja na kuendeleza majadiliano ya kidini na kiekumene, ili kujenga umoja na urafiki kati ya watu wa mataifa.

Baba Mtakatifu anahitimisha hotuba yake kwa kuwataka wanajumuiya ya Mtakatifu Egidio kujikita katika maisha ya sala, huduma makini kwa maskini pamoja na kuendelea kuwa ni wajenzi wa amani na upatanisho sehemu mbali mbali za dunia. Hii ni chemchemi ya mageuzi ndani ya jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.