2014-06-14 07:01:58

Sherehe ya Jamhuri ya Muungano!


Kitendawilitega cha kiswahili, “tatu tatu mpaka pwani,” ni rahisi sana kukitegua kwa wapishi wa jiko la kienyeji, kwani watayakumbuka mara moja mafiga matatu yanayotegemeza chungu jikoni. Kumbe kwa asiye mkristo anaposikia juu ya Sikukuu ya Utatu Mtakatifu anaona hiyo kuwa ni kufuru nzito sana kwa Mungu isiyostahili msamaha.

Aidha kwetu Wakristo, sikukuu hii inaonekana kuwa ni kitendawilitega kikuu cha imani kisicho na jibu wala na mteguaji. Tunabaki kusema kuwa hilo ni “Fumbo la Imani”. Aidha kama Utatu upo, basi sikukuu hii ni ya Utatu Mtakatifu hainihusu mimi na iko mbali sana nasi na haigusi kabisa maisha yetu.

Ama kweli “Jambo usilolijua litakusumbua”. Ndugu zangu, Sikukuu ya Utatu siyo kitendawilitega, tena basi ni sikukuu yako kabisa. Jibu na mteguaji wa kitendawili cha Sikukuu ya leo ni wewe mwenyewe, wala usiepe majukumu. Hoja ni kwamba, ukifanya tafakari ya maisha yako kwa dhati utagundua mara moja kuwa sikukuu hii ni yako wewe. Yaani, ni sikukuu inayotokana na mang’amuzi ya maisha yako na katika ulimwengu wako huu. Utatu ni ukweli halisi unaouishi binadamu lakini kwa bahati mbaya pengine hatuufanyii tafakari. Mapato yake unabaki kuwa kama uliyelibeba shoka begani huku unajisumbua kulitafuta ukipita kuliuzia kwa wengine.

Ukipata kitendawili kama hiki: “Sikukuu ya Utatu ni nini? Wewe jibu kwanza kirahisi tu kuwa ni Sikukuu ya “Muungano” au “Jamhuri ya Muungano”. Jamhuri ni neno la kiarabu lenye maana ya watu, au taifa na kwa kiingereza ni public, au – republic linalotokana na maneno mawili ya la kilatini – res (vitu, mali, raslimali, tunu) na – publicum (watu, umma, taifa). Kwa hiyo Jamhuri – republic, ni kuunganisha raslimali ya watu na taifa au maamuzi ya watu au ya taifa kuwa ya umma. Katika uwanja wa siasa Jamhuri ya Muungano – United Republic humaanisha muunganiko wa mataifa mawili au zaidi na raslimali zao za umma na kufanya kuwa Taifa moja.

Kwetu sisi, Sikukuu ya leo ya Fumbo la Utatu Mtakatifu ni ufunuo au ufumbuzi wa siri ya maisha, ni chemchemi ya hekima ya maisha ambayo msingi wake ni kuelewa uhusiano, umoja wa mambo, wa hali, wa nafsi nk. Kwa hiyo tungeweza kusema kuwa leo ni sikukuu ya “Muungano.” Kimsingi na kwa uasili wake, kipeo cha muungano wowote ule kinatokana na muungano wa kifumbo ulio katika Mungu.

Lakini awali ya yote budi ieleweke kuwa Mungu ni mmoja tu, hakuna Mungu wawili au watatu au zaidi. Halafu, yabidi uelewe na utoe maelezo kwamba Mungu huyu kwa yeye mwenyewe siyo jiwe lisilo na uhai, bali anazo sifa nyingi sana zilizoungana katika yeye, yaani Mungu ni tajiri sana na mwingi wa raslimali zilizoungana katika yeye na mwenye makakala – nguvu (dynamic).

Kwa hiyo, Mungu siyo “upweke” bali ni “muungano”. Aidha, makakala (dynamism) hayo katika Mungu yanaunganishwa na upendo ulio wa milele katika yeye. Kwa hiyo ukitaka kumwelewa Mungu na utajiri wake unaounganishwa na upendo, usitumie njia ya kiakili au njia ya kiutaalamu au ya kidhahania (kimawazo), bali tumia njia ya mang’amuzi ya maisha ya kawaida kabisa, yaani wewe umtazame binadamu, umfanyie fikara na umtafakari kidhati binadamu jinsi alivyo “muungano” wa mambo makuu katika yeye.

Kwa hiyo “fumbo umfumbie mjinga” kwa sababu jibu la fumbo hili unalipata kwa wewe binadamu mwenyewe. Tukifajitafakri kidogo tu, tutagundua kirahisi kwamba, binadamu kwanza anayo maisha, uzima au uhai ambao tunajua tumeupata toka kwa Mungu aliyetuumba; pili, katika maisha hayo, tutagundua kuwa binadamu tunahitaji upendo, yaani kujipenda, kupenda na kupendwa na wengine ili tuweze kuendeleza maisha. Tatu, tutagundua pia kwamba, katika binadamu kuna hatima ya maisha tuliyopangiwa na Mungu, yaani mwisho wa maisha yetu ambayo siyo kifo tu, bali tutaendelea kuishi na Mungu aliyetuumba.

Ili tuweze kuelewa kiundani muungano wa hali hizi tatu, tunaweza kusema kwamba utatu ni hekima au busara ya kujua ni kitu gani hayo maisha, uhai na uzima; halafu ni busara ya kujua ni nini huo upendo; na mwisho ni busara ya kutambua ni nini hatima au mwisho wa binadamu. Kwa hiyo, endapo Utatu ni hekima ya maisha, ya upendo na ya kifo, basi Utatu huu unafaa kuutathmini kwa sababu unaeleza hali halisi ya uwepo wa binadamu. Hebu sasa tuuangalie muungano huo katika binadamu kisha tuulinganishe na Sikukuu ya muungano wa Utatu Mtakatifu tunayosherekea leo, tukiongozwa na Injili ya leo.

Utatu ni Uzima, au Uhai wenye asili yake kwa Mungu:
Hapo mwanzo Mungu alipotaka kumwumba binadamu alisema: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu” (Mwanzo 1:26). Mungu ametupa uhai, maisha na uzima (ametuumba) na tunafanana naye. Kwa hiyo, Mungu ni utajiri wa uhai na uzima alio nao hadi akasema: “tufanye”, na utajiri huo wa uzima ametushirikisha sisi kwa kutuumba.

Aidha kufanana kwetu naye siyo na Mungu mwumbaji au na Roho au na Neno la milele, bali ni utajiri wa uhalisia huo wote wa Mungu kijumla. Ni muungano au uhusiano ambao ni msingi wa ndani kabisa wa Mungu na binadamu. Mtu ameumbwa kwa mfano wa mahusiano na wa muunganiko huo. Kwa sababu upweke ni kinyume na hali aliyoumbwa nayo binadamu upweke huo unatisha na hauvumiliki. Ndiyo maana ninapokaa pamoja na wengine ninajisikia vizuri, kwani huo ndiyo wito wangu.

Kwa hiyo kama Mungu wetu asingekuwa na utajiri uhai ulioungana hadi akajitoa zawadi, tusingeshirikishwa uhai wake na tusingeweza kufanana naye na hivi huyo asingekuwa Mungu, badala yake angekuwa Mungu wa kufikirika na wa kidhahania tu. Kumbe huyo siyo Mungu wa kimawazo, bali daima anajitoa, daima anatukirimu, daima anatoka na kutujia ili kuwa nasi. Mungu huyo yupo daima katika harakati.

Utatu ni Upendo wenye asili yake kwa Mungu
Bila upendo hakuna muungano na ushirikiano na wala hakuna umoja. Kwa hiyo utatu ni muungano wa upendo, ambao Injili inatangaza wazi leo: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanae wa pekee” (Yoh. 3:16). Aya hiyo ndiyo kiini cha Injili ya Yohane anayesema: “Mungu ni upendo” (IYoh 4:8-16) na anatutaka sote tukiri na kusema kwa kustaajabia: “Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini.

Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake.” (IYoh. 3:16). Kwa hiyo watu wanapokuuliza wewe mkristu: “unasadiki nini?” Jibu tunalotegemea daima ni lile la kutoka kitabu cha katekisimu ya kanisa: “Nasadiki kwa Mungu Baba Mwenyezi muumba mbingu na dunia; na kwa Yesu Kristu Mwanae wa pekee, aliyesulibiwa na kufufuka. Nasadiki kwa kanisa moja takatifu….” nk.

Ni sawa kabisa jibu hilo. Lakini swali hilo hilo ukimwuliza yeyote asiye mkristu “Wewe unasadiki nini hapa duniani?” Utapata majibu mengi sana na mwingine atakuambia “mimi sisadiki Mungu” wakati hujamwuliza swali la Mungu. Lakini jibu moja linaloweza kutolewa na wote bila kujali itikadi zao za dini au uraia, utamaduni wala elimu, ni kwamba binadamu yeyote yule anasadiki juu ya Upendo. Hilo ndilo jambo muhimu, kwa sababu kila mtu, kila kiumbe, hata asiyesadiki chochote au asiye mwamini anaweza kulisadiki pendo, anaweza kujiaminisha au kusadiki juu ya upendo kama ndiyo busara pekee ya maisha.

Asiyesadiki juu ya upendo huyo yuko katika laana ya maisha yasiyo na uzuri wowote. Ndivyo hivyo anavyotuambia Yohane “Sisi tumesadiki juu ya upendo.” Ukisadiki katika utajiri ulio katika upendo, hapo unakumbana na Jamhuri nyingine ya muungano, kwani tendo la kupenda daima linaenda pamoja na tendo jingine zito nalo ni kutoa.

Kwa hiyo, kupenda ni sawa na kutoa au kujitoa. Huwezi kutoa usichokuwa nacho – nemo dat quod non habet. Kama unatoa maana yake una kitu cha kugawa. Mungu anapenda kwa vile anatoa, hivi Mungu amefurika upendo. Mwinjili anatuambia: “Mungu aliupenda sana ulimwengu hata akamtoa Mwanae wa pekee.” Utajiri mkuu wa Mungu ndiyo Upendo ambao ni Yesu Kristu aliye Mungu. Yohane anasema tena “Mungu aliupenda mno ulimwengu.” Hakumpenda binadamu peke yake bali aliupenda pia ulimwengu, dunia, wanyama, mimea na uumbaji wote kijumla. Mungu ametoa uhai kwa wote bila ubaguzi. Endapo yeye ameupenda ulimwengu, nami pia yanibidi kuipenda dunia hii, watoto wake, mimea, maua, nk. Kwa hiyo, katika upendo tusijiulize tunaweza kupokea nini toka kwa wengine, bali tujiulize sisi tunaweza kutoa nini kwa wengine.

Utatu ni Hatima yenye mwanzo na mwisho (Alfa na Omega) kwa Mungu siyo hukumu.
“Mungu hakumtuma Mwanae ulimwenguni ili kuuhukumu, bali kusudi ulimwengu uokolewe.” Maana ya kuokoa ni kuwa na fikra potovu na ya kutisha ya “Kufabasi”. Kifo siyo hatima yetu, bali hatima yetu ni kukaa na Mungu. Mungu anapenda kuokoa, kutoa maisha, kutufanya sisi sote kuwa watoto wake. Mungu anatoa maisha yake, anataka kutukomboa sote tuwe waana katika Mwana, na tuendelee kuishi naye milele. Yohane anatutaka tusafishe fikra mbovu tulizo nazo juu ya Mungu, anataka kutuondolea woga juu ya Mungu yaani tutoe picha ya Mungu aliye mkali na anayeadhibu na kwamba kifo siyo hatima yetu ya mwisho.

Kwa hiyo, sikukuu ya utatu ni kioo cha undani wa moyo wangu kinachonionesha nimetoka wapi, niko wapi na hatima yangu na ya ulimwengu huu ni ipi. Siku ya leo ni sawa na kusherekea kwa pamoja sikukuu tatu za maisha yangu, yaani kuzaliwa (uzima, uhai, maisha), ndoa (mwito wowote – upendo) na kifo (hatima, umilele). Kwa hiyo Utatu ni Mungu aliye Uzima wote, Upendo wote na asiye na hatima, Anadumu milele yote. Sisi pia tunatembea katika Muungano huo na tupo safarini kuelekea umilele (hatima) usiyo na mwisho, kwenye Jamhuri ya Muungano Mtakatifu. Kumbe leo ni Sherehe ya Jamhuri ya Muungano wa undani wangu, maisha yangu, upendo wangu na hatima yangu. Asili ya muungano huo ni utajiri mkuu wa muungano ulio katika Utatu Mtakatifu wa Mungu Mmoja. Heri kwa Sikukuu ya Utatu Mtakatifu.

Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.