Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani katika mkutano wake wa mwaka uliofunguliwa hapo
tarehe 11 hadi tarehe 13 Juni 2014 huko New Orleans umejadili pamoja na mambo mengine
umuhimu wa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia,
kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya, changamoto inayofanyiwa kazi na Mama
Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo!
Mada hii inakwenda
sanjari na maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu Katoliki kuhusu
familia itakayoadhimishwa mwezi Oktoba mjini Vatican. Haya pia ni maandalizi ya Siku
ya Familia Duniani itakayoadhimishwa Jimbo kuu la Philadelphia hapo Septemba 2015
na Baba Mtakatifu Francisko amealikwa kuhudhuria tukio hili linaloonesha vipaumbele
vya kichungaji kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa nyakati hizi.
Matukio
yote mawili ni fursa muhimu sana kwa Kanisa kupembua kuhusu: tunu msingi za maisha
ya ndoa na familia; dhamana na utume wa familia katika maisha ya Kanisa na mchango
wa familia katika kuimarisha mahusiano ya kijamii.
Akichangia mada kuhusu familia
kwenye mkutano wa Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, Askofu mkuu Vincenzo Paglia,
Rais wa Baraza la Kipapa la familia anabainisha kwamba, lengo la maadhimisho ya Siku
ya Familia Duniani ni kuonesha upendo ambao mwanadamu anapaswa kuoneshwa na kushirikishwa.
Injili ya Familia haina budi kuvuka mipaka ya ubinafsi na upweke katika maisha ya
watu.
Waamini na watu wote wenye mapenzi mema ndani na nje ya Marekani wanahamasishwa
na Mama Kanisa kushiriki katika matukio yote haya mawili kwa uwepo wao mkalimifu au
kwa njia ya sala. Maadhimisho haya kwa Marekani itakuwa ni fursa ya kutangaza Injili
ya Furaha pamoja na kupyaisha maisha ya ndoa na familia. Waamini watapata fursa ya
kutafakari asili ya ndoa na familia kadiri ya mpango wa Mungu kwa mwanadamu; mafundisho
tanzu kuhusu ndoa na familia kadiri ya Kanisa Katoliki.
Askofu mkuu Paglia
anasema kwamba, kuna uhusiano mkubwa kati ya imani na kumong'onyoka kwa tunu msingi
za maadili na utu wema; kwani hapa mtu binafsi na haki zake binafsi anapewa kipaumbele
cha kwanza kuliko tunu msingi na haki za familia. Kuna baadhi ya nchi zinatunga sheria
kwa kuzingatia mahitaji ya mtu binafsi na kuzitenga familia katika mchakato huu.
Kutokana
na mantiki hii inaonekana kwamba, familia sehemu mbali mbali za dunia zinaendelea
kubezwa kana kwamba hazina mchango mkubwa katika ustawi na maendeleo ya watu. Kuna
sehemu ambako familia zinaendelea kunyanysika na kudhulumiwa kisheria! Zote hizi ni
changamoto katika maisha ya ndoa na familia! Mazingira yote haya yanapelekea watu
kupendelea zaidi upweke kuliko kufanya maamuzi ya kuanzisha familia.
Lakini
familia inayojadiliwa na kupigiwa debe na Mama Kanisa ni kadiri ya mpango na utashi
wa Mungu kwa binadamu na wala si vinginevyo! Familia itaendelea kuwa ni rasilimali
kubwa katika ustawi na maendeleo ya Jamii.