2014-06-13 09:04:18

Maskini ni kiini cha Injili!


Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Fumbo la Utatu Mtakatifu kielelezo cha mshikamano wa upendo Jumapili jioni tarehe 15 Juni 2014 anatarajiwa kutembelea Jumuiya ya Mtakatifu Egidio kwenye makao yake makuu yaliyoko kwenye Kanisa la Bikira Maria wa Trastevere mjini Roma.

Lengo la hija hii ya kichungaji ya Baba Mtakatifu ni kukutana na kuzungumza na maskini na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kutokana na hali yao ya maisha, kwani hawa ndio kiini cha Habari Njema, changamoto kubwa inayofanyiwa kazi na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio kwa kujipambanua kwa huduma makini kwa maskini!

Akiwa Kanisa hapo, Baba Mtakatifu ambaye ana ibada ya pekee kwa Bikira Maria, atatoa heshima zake za dhati kwa Sanamu ya Bikira Maria; atasikiliza shuhuda kutoka kwa maskini wanaohudumiwa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio mjini Roma na baadaye atawapatia neno la faraja, imani na matumaini. Kutakuwa na muda maalum kwa ajili ya kusali na kumshukuru Mungu kwa wema na ukarimu wake katika maisha ya watu.

Baba Mtakatifu atapata fursa pia ya kuzungumza na viongozi wakuu wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio pamoja Familia ya Mtakatifu Egidio inayoundwa na Makleri pamoja na waamini walei. Hii ni Jumuiya inayoendelea kuwa kweli ni shule ya amani, huduma kwa maskini, wageni na wahamiaji. Maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ni kiini cha dhamana na utume wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio. Baba Mtakatifu Yohane Paulo II, Papa mstaafu Benedikto XVI ni kati ya Mapapa ambao wametembelea na kusali pamoja na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio.







All the contents on this site are copyrighted ©.