Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Fumbo la Utatu Mtakatifu kielelezo
cha mshikamano wa upendo Jumapili jioni tarehe 15 Juni 2014 anatarajiwa kutembelea
Jumuiya ya Mtakatifu Egidio kwenye makao yake makuu yaliyoko kwenye Kanisa la Bikira
Maria wa Trastevere mjini Roma.
Lengo la hija hii ya kichungaji ya Baba Mtakatifu
ni kukutana na kuzungumza na maskini na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kutokana
na hali yao ya maisha, kwani hawa ndio kiini cha Habari Njema, changamoto kubwa inayofanyiwa
kazi na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio kwa kujipambanua kwa huduma makini kwa maskini!
Akiwa
Kanisa hapo, Baba Mtakatifu ambaye ana ibada ya pekee kwa Bikira Maria, atatoa heshima
zake za dhati kwa Sanamu ya Bikira Maria; atasikiliza shuhuda kutoka kwa maskini wanaohudumiwa
na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio mjini Roma na baadaye atawapatia neno la faraja, imani
na matumaini. Kutakuwa na muda maalum kwa ajili ya kusali na kumshukuru Mungu kwa
wema na ukarimu wake katika maisha ya watu.
Baba Mtakatifu atapata fursa pia
ya kuzungumza na viongozi wakuu wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio pamoja Familia ya Mtakatifu
Egidio inayoundwa na Makleri pamoja na waamini walei. Hii ni Jumuiya inayoendelea
kuwa kweli ni shule ya amani, huduma kwa maskini, wageni na wahamiaji. Maskini na
wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ni kiini cha dhamana na utume wa Jumuiya ya
Mtakatifu Egidio. Baba Mtakatifu Yohane Paulo II, Papa mstaafu Benedikto XVI ni kati
ya Mapapa ambao wametembelea na kusali pamoja na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio.