Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe 12 Juni, inaadhimisha Siku ya Kimataifa
dhidi ya kazi za suluba kwa watoto wadogo! Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya
Katekesi yake Jumatano tarehe 11 Juni 2014 alilizungumzia tatizo hili ambalo linaendelea
kuwadhulumu, kuwanyonya na kuwanyanyasa watoto kwa kuwafanyisha kazi katika mazingira
magumu na hatarishi; kiasi kwamba, wengi wao wanageuzwa kuwa ni watumwa na hata wakati
mwingine kubaguliwa!
Baba Mtakatifu Francisko anaiomba Jumuiya ya Kimataifa
kusimama kidete kuwalinda, kuwatetea na kuwanusuru watoto kutoka katika janga hili
la maisha. Kila mtu ndani ya jamii, lakini zaidi, familia ziendelee kuwajibika barabara,
ili kulinda na kutetea utu na heshima ya kila mtoto, ili aweze kupata malezi na makuzi
bora. Utoto mtulivu unawahakikishia watoto maisha bora zaidi kwa siku za usoni. Baba
Mtakatifu aliwaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema waliokuwepo kwenye Uwanja
wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican Jumatano asubuhi kusali kwa ajili ya
kuwaombea watoto wanaodhalilishwa na kunyanyaswa utu na heshima yao!
Shirika
la Kazi Duniani (ILO) linakadiria kwamba, kuna zaidi ya watoto millioni 168 wanaofanyishwa
kazi za suluba sehemu mbali mbali za dunia. Umoja wa Mataifa unataka kufuta janga
hili kwenye uso wa dunia ifikapo mwaka 2016. Kazi za suluba ni chanzo kikuu cha kudumaa
kwa watoto wadogo, kiasi kwamba afya zao zinaathirika vibaya kwa kunyimwa usalama
na makuzi stahiki. Asilimia kubwa ya watoto wanaofanyishwa kazi za suluba wako Barani
Asia.
Kusini mwa Jangwa la Sahara, watoto zaidi ya millioni 59, wengi wao wakiwa
wanatoka Burundi wanafanyishwa kazi za suluba hasa majumbani. Maadhimisho ya Siku
hii kimataifa ni kutaka kuibua sera na mikakati itakayosaidia kudhibiti tabia ya kuwafanyisha
kazi za suluba watoto wadogo, changamoto kwa familia kutekeleza wajibu na dhamana
yao bila kusita. Serikali zikiwa na sera makini zinaweza kusaidia familia zenye kipato
cha chini kumudu gharama za maisha; kwa kupata huduma msingi za elimu na afya.