2014-06-13 08:13:46

Bajeti ya Serikali ya Tanzania


Wizara ya fedha nchini Tanzania, Alhamisi tarehe 12 Juni 2014 imesoma makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka 2014/2015 huku ikiahidi kuendelea kuongeza kima cha chini cha mishahara ya watumishi wa umma. Mbali ya kuongeza mishahara hiyo pia katika mwaka wa fedha wa 2014/2015 imepanga kufanya marekebisho katika mfumo wa kodi ya mishahara (PAYE) kwa kupunguza kiwango cha kodi hadi kufikia kima cha chini cha asilimia 12% kutoka asilimia 13%.
Hatua hiyo inalenga katika kutoa unafuu wa kodi kwa wafanyakazi na serikali itaendelea kupunguza kiwango hicho hatua kwa hatua ili kuwapa nafuu zaidi ya kodi wafanyakazi.

Akisoma bajeti hiyo, Waziri wa Fedha Saada Salum Mkuya alisema uchumi umeendelea kukua kwa kiwango cha kuridhisha na ukuaji huo umeongeza pato halisi la kila mtanzania hadi kufikia sh. 1,186,200 mwaka 2013 kutoka sh. 1,025,038 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 14%. Waziri alisema pia umasikini wa kipato umeendelea kupungua ambapo kwa mujibu wa takwimu mpya za utafiti umeonyesha kuwa umasikini wa kipato umepungua kwa wastani wa asilimia 6.2% kati ya mwaka 2007 na 2012. Akizungumzia mfumuko wa bei nchini Waziri alisema umeendelea kushuka kutoka asilimia 9.4% April 2013hadi kufikia asilimia 6.3% April 2014. Alisema lengo la serikali hadi kufikia Juni, 2014 mfumuko wa bei ufikie asilimia 6% lengo ambalo linatarajiwa kufikiwa.

Alisema kupungua kwa kasi ya upandaji bei kulitokana na sera madhubuti za fedha, hali nzuri ya hewa na jitihada za serikali kuongeza ruzuku ya pembejeo za kilimo na hivyo kuongeza uzalishaji wa mazao. Aidha Waziri Saada alisema serikali inalenga kurekebisha viwango maalumu vya ushuru wa bidhaa zisizokuwa za mafuta kwa kwa asilimia 10% kwa bidhaa kama vinywaji baridi, mvinyo, pombe, vinywaji vikali ushuru wa vinyawaji baridi.

Waziri alisema bidhaa za sigara zitatozwa ushuru wa bidhaa wa asilimia 25% ili kutekeleza matakwa ya mkataba wa udhibiti wa matumizi ya tumbaku wa Shirika la Afya Duniani. Alisema ushuru wa vinywaji baridi umeongezeka kutoka sh, 91 kwa lita hadi kufikia sh. 100 kwa lita ikiwa ni ongezeko la shilingi 9. Waziri alisema ushuru wa bidhaa kwenye maji ya matunda iliyotengenezwa na matunda yanayozalishwa hapa nchini imeongezeka kutoka asilimia 9% kwa lita hadi asilimia 10%.

Alisema ushuru wa bia inayotengenezwa kwa nafaka ya hapa nchini na ambayo haijaoteshwa kama vile Kibuku imepanda kutoka sh. 341% kwa lita hadish. 375%.
Huku ushuru wa bia nyingine zote ushuru umepanda kutoka sh. 578 kwa lita hadi kufikia 635 kwa lita ikiwa ni ongezeko la sh. 57 kwa lita. Kwa upande wa ushuru wa mvinyo uliotengenezwa kwa Zabibu unaozalishwa nchini kwa kiwango kinachozidi asilimia 75% , Saada alisema umepanda kutoka sh. 160 kwa lita hadi sh.176 kwa lita.

Alisema kwa mvinyo unaozalishwa kwa Zabibu ambao hauzalishi hapa nchini kwa kiwango kinachozidi asilimia 25% ushuru umeongezeka kutoka sh. 1,775 kwa lita hadi kufikia sh.1,953 kwa lita. Vinywaji vikali ushuru umeongezeka kutoka sh.2,631 kwa lita hadi sh. 2,894 kwa lita ikiwa ni ongezeko la sh. 263.

Waziri alisema ongezeko jingine la ushuru ni kwa bidhaa ya sigara zisizo na vichungi zinazotengenezwa kutokana na Tumbaku inayozalishwa hapa nchini kwa kiwango cha angalau asilimia 75% kutoka sh.9,031 hadi Sh.11,289 kwa sigara 1000. Alisema kwa upande wa sigara zinzotengenezwa hapa nchini kwa kiwango cha angalau asilimia 75% ushuru umeongezeka kutoka sh.21,351 hadi sh.26,689 kwa sigara 1,000.

Saada alisema sigara nyingine zenye sifa tofauti na hizo suhuru umeongezeka kutoka sh.38,628 hadi sh.48,285 kwa sigara 1,000 ikiwa ni ongezeko la sh.9,657 sawa na sh.9.65 kwa sigara moja.

Alisema hatua hizo katika ushuru wa bidhaa kwa pamoja zinatarajiwa kuongeza mapato ya serikali kwa kiasi cha sh. milioni 124,292. Pia Waziri huyo alisema utaratibu wa utozaji wa kodi ya mafuta ya petrol unaotumika hivi sasa ni wa kuchelewesha malipo ambapo kodi inakadiriwa na baada ya kukadiria malipo hufanyika katika siku 45. Alisema Tanzania ni nchi pekee inayotumia utaratibu huo katika nchi za Afrika Masharikia ambapo utaratibu huo hutoa mwanya wa ukwepaji wa kodi na hivyo Waziri Saada alipendekeza kuwa mara baada ya kodi kukadiriwa ilipwe mara moja.


Wakati huo huo Serikali ya Tanzania imesema imeandaa mapendekezo ya sheria ambayo itafikishwa bungeni ili kuangalia ni uwekezaji wa aina gani unahitaji misamaha ya kodi na ipi haitaji. Kauli hiyo ilitolewa alhamisi tarehe 12 Juni 2014 bungeni na Waziri Mkuu Mizengo Pinda alipokuwa akijibu swali la papo kwa papo la Murtza Mangungu (Kilwa Kaskazini-CCM). Katika swali lake Mangungu alitaka kujua nini kauli ya serikali juu ya misamaha ya kodi wanayopewa wawekezaji kwani sasa imekuwa ni chungu kwa viwanda vya ndani.

Pinda alisema suala la misamaha ya kodi lilitolewa makusudi ili kuwawezesha wawekezaji kuwekeza kwa manufaa makubwa ya nchi hapo baadae. Alisema baadhi ya wawekezaji wamekuwa wakiitumia vyema misamaha hiyo lakini pia wapo ambao hawatumii vizuri. Alisema hata hivyo mamlaka ya Mapato TRA na vyombo vingine vimekuwa vikifuatilia kwa karibu wawekezaji ambao wamepata misamaha ya kodi lakini bado kuna umuhimu wa kuimarisha zaidi usimamizi.

Pinda alisema ipo hofu kuwa misamaha hiyo inaweza kuua viwanda vya ndani kutokana na wawekezaji kusamehewa kodi kwa muda mrefu huku wakizalisha bidhaa ambazo zinazalishwa hapa nchini. Pinda alisema serikali imeliona hilo na kwa sasa inaendelea kulidhibiti ikiwemo kuimarisha viwanda vya ndani ikiwemo vya ngozi, sukari na bidhaa nyingine.

“Misamaha katika viwanda kama vya sukari, saruji vya kutoka nje ni vyema ikafutwa ili kuvipa viwanda vyetu nguvu zaidi’’ alisema “Haiwezekani tuwe tunanunua kanga kila wakati toka nje dawa ni kupiga ushuru mkubwa ili viwanda vyetu navyo vifanye vizuri hilo nalo tunaliangalia.’’ Alisema heshima ya nchi yeyote Duniani ni kuwa na viwanda vyake yenyewe na si kutegemea viwanda vya nje. Aidha Pinda alisema Wizara ya Kazi na Ajira pamoja na Uhamiaji wametakiwa kutoruhusu ajira za wageni ambazo watanzania wanaweza kuzifanya.

Pinda alisema Serikali imekuwa macho katika kukataza wageni toka nje kuja kufanya kazi nchini ambazo watanzania wanaweza kuzifanya kwani kwa kufanya hivyo ni kuwanyima fursa wazawa.

Alisema pale aina ya uwekezaji unapohitaji wafanyakazi kutoka nje basi wataruhusiwa kufanya hivyo lakini ni lazima watanzania kiasi fulani wawepo. ‘’Nilikwenda pale Mtwara Dangote niliona Yule mwekezaji akiwa na wafanyakazi toka nje lakini wapo vijana wakitanzania wakifanya kazi huku wakijifunza na hata katika Bomba la gesi pia wapo wachina lakini watanzania nao wapo.’’ Alisema.

Akizungumzia kuhusiana na wageni kuja kufanya biashara ndogo ndogo nchini Waziri Mkuu alisema hali hiyo inatokaka na kutokuwepo kwa viwanda vya kutosha hapa nchini. Alisema kutokana na nchi kuwa mchuuzi wa kila kitu kumewafanya wafanyabiashara wengi kukimbilia Tanzania huku wakiwemo walioruhusiwa kisheria na hata wale ambao hajaruhusiwa.

Kwa mujibu wa Pinda ni vyema sasa kukawa na mkakata wa makusudi wa kuzalisha bidhaa mbalimbali hapa hapa nchini ili kulinda viwanda vya ndani. Alisema katika kulinda viwanda vya ndani ni bora kuweka kodi kubwa kwa bidhaa za nje zinazoweza kuzalishwa hapa nchini ili kupunguza uingizaji wake. “Hata kama kuna mfanyabiashara analeta bidhaa hapa nchini dawa ni kumbana tu ajenge kiwanda hicho hapa hapa nchini ili azalishe bidhaa zake’’ alisema.

Na wakati huo huo WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amesema si dhambi kwa watanzania waliosomeshwa na fedha za walipa kodi kwenda kufanya kazi nje ya nchi. Pinda aliyasema hayo alipokuwa akijibu swali la Rashid Ali Abdalah (Tumbe-CUF) aliyetaka kujua ni kwanini serikali inaruhusu vijana waliosomeshwa kwa gharama kubwa kwenda kufanya kazi nje ya nchi.

Alisema ni muhimu kwa vijana wa aina hiyo wakatiwa moyo kwenda kufanya kazi nje lakini baada ya muda warejee nchini wakiwa na ujuzi zaidi. Pinda alisema serikali imeliona tataizo hilo na kwa sasa wameendelea na sera mbalimbali ambazo zitaweza kuwabakisha vijana hao hapa nchini badala ya kukimbilia nje ya nchi. “Kwa kweli kinachowafanya vijana hawa kukimbilia nje ni mishahara hivyo kutokana na sera zetu tunaangalia jinsi ya kuongeza mishahara hivyo nadhani itasaidia kuwafanya wabaki hapa nchini.

Aidha Waziri Mkuu alisema tatizo la ajira kwa vijana waliohitimu masomo si tatizo la Tanzania pekee bali ni tatizo linalozikumba nchi nyingi.

Alisema kwa kupitia juhudi zinazofanywa na Chama cha Mapinduzi CCM tatizo hilo huenda likapata ufumbuzi katika muda mfupi ujao. Alisema kwa sasa serikali imekuwa ikijitahidi kuwaajiri wahitimu mbalimbali moja kwa moja wakiwemo walimu na watalaamu katika fani mbali mbali za maisha. Pinda alisema sehemu nyingine ambao inaweza kuajiri wahitimu wengi ni sekta binafsi na pia vijana kutumia fursa zilizopo ili kujiajiri. Kwa mujibu wa Pinda fursa zingine ni ukanda wa kiuchumi wa EPZ nalo ni sehemu ya kukabiliana na tatizo la ajira.

Pia Waziri mkuu Pinda katika kipindi hicho alisema kuwa serikali haitaruhusu Chuo Kikuu cha UDOM kukataza wanafunzi 500 kufanya mitihani yao ya mwisho kwa kuwa hawajalipa ada. Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyasema hayo alipokuwa akijibu swali la Haji Khatib Kai (Micheweni-Cuf) aliyetaka kujua nini kauli ya serikali juu ya hatma ya wanafunzi hao ambao wameambiwa hawatafanya mitihani kutokana na kutolipa ada.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu kuna taarifa kuwa kuna wanafunzi zaidi ya 500 wa Chuo Kikuu cha UDOM watazuiliwa kufanya mitihani yao kutokana na kukosa ada na hawa ni watoto wa masikini nini kauli ya serikali katika hili.’’ Alisema. Akijibu swali hilo Pinda alisema serikali haitaruhusu vijana hao kukosa kufanya mitihani yao kutokana na ada. Alisema vijana hao wamesoma kwa miaka mitatu hivyo suala la ada haliwezi kuwa sababu ya kupoteza muda wao wote.

“Tutajitahidi vijana hao watafanya mitihani yao kama ilivyopangwa , sidhani kama kutakuwa na tatizo na hawa vijana mara nyingi wakiwa na jambo huja kwangu kuniambia lakini kwa hili hili hawajafika.’’ Alisema. Waziri Mkuu Pinda alisema serikali itaendelea kuzuia kufanyika kwa mikutano ya hadhara katika mikoa ya Mtwara na Lindi mpaka hapo itakapojiridhisha na hali ya usalama na utulivu katika mikoa hiyo. Waziri Mkuu alisema kwa sasa bado wanaendelea kufutilia hali hiyo kwani hivi karibuni walishataka kutoa ruhusa kwa mkoa wa Lindi lakini hali ilikabadilika.








All the contents on this site are copyrighted ©.