Wizara ya fedha nchini Tanzania, Alhamisi tarehe 12 Juni 2014 imesoma makadirio ya
mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka 2014/2015 huku ikiahidi kuendelea kuongeza
kima cha chini cha mishahara ya watumishi wa umma. Mbali ya kuongeza mishahara hiyo
pia katika mwaka wa fedha wa 2014/2015 imepanga kufanya marekebisho katika mfumo wa
kodi ya mishahara (PAYE) kwa kupunguza kiwango cha kodi hadi kufikia kima cha chini
cha asilimia 12% kutoka asilimia 13%. Hatua hiyo inalenga katika kutoa unafuu wa
kodi kwa wafanyakazi na serikali itaendelea kupunguza kiwango hicho hatua kwa hatua
ili kuwapa nafuu zaidi ya kodi wafanyakazi.
Akisoma bajeti hiyo, Waziri wa
Fedha Saada Salum Mkuya alisema uchumi umeendelea kukua kwa kiwango cha kuridhisha
na ukuaji huo umeongeza pato halisi la kila mtanzania hadi kufikia sh. 1,186,200 mwaka
2013 kutoka sh. 1,025,038 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 14%. Waziri alisema
pia umasikini wa kipato umeendelea kupungua ambapo kwa mujibu wa takwimu mpya za utafiti
umeonyesha kuwa umasikini wa kipato umepungua kwa wastani wa asilimia 6.2% kati ya
mwaka 2007 na 2012. Akizungumzia mfumuko wa bei nchini Waziri alisema umeendelea kushuka
kutoka asilimia 9.4% April 2013hadi kufikia asilimia 6.3% April 2014. Alisema lengo
la serikali hadi kufikia Juni, 2014 mfumuko wa bei ufikie asilimia 6% lengo ambalo
linatarajiwa kufikiwa.
Alisema kupungua kwa kasi ya upandaji bei kulitokana
na sera madhubuti za fedha, hali nzuri ya hewa na jitihada za serikali kuongeza ruzuku
ya pembejeo za kilimo na hivyo kuongeza uzalishaji wa mazao. Aidha Waziri Saada alisema
serikali inalenga kurekebisha viwango maalumu vya ushuru wa bidhaa zisizokuwa za mafuta
kwa kwa asilimia 10% kwa bidhaa kama vinywaji baridi, mvinyo, pombe, vinywaji vikali
ushuru wa vinyawaji baridi.
Waziri alisema bidhaa za sigara zitatozwa ushuru
wa bidhaa wa asilimia 25% ili kutekeleza matakwa ya mkataba wa udhibiti wa matumizi
ya tumbaku wa Shirika la Afya Duniani. Alisema ushuru wa vinywaji baridi umeongezeka
kutoka sh, 91 kwa lita hadi kufikia sh. 100 kwa lita ikiwa ni ongezeko la shilingi
9. Waziri alisema ushuru wa bidhaa kwenye maji ya matunda iliyotengenezwa na matunda
yanayozalishwa hapa nchini imeongezeka kutoka asilimia 9% kwa lita hadi asilimia 10%.
Alisema
ushuru wa bia inayotengenezwa kwa nafaka ya hapa nchini na ambayo haijaoteshwa kama
vile Kibuku imepanda kutoka sh. 341% kwa lita hadish. 375%. Huku ushuru wa bia
nyingine zote ushuru umepanda kutoka sh. 578 kwa lita hadi kufikia 635 kwa lita ikiwa
ni ongezeko la sh. 57 kwa lita. Kwa upande wa ushuru wa mvinyo uliotengenezwa kwa
Zabibu unaozalishwa nchini kwa kiwango kinachozidi asilimia 75% , Saada alisema umepanda
kutoka sh. 160 kwa lita hadi sh.176 kwa lita.
Alisema kwa mvinyo unaozalishwa
kwa Zabibu ambao hauzalishi hapa nchini kwa kiwango kinachozidi asilimia 25% ushuru
umeongezeka kutoka sh. 1,775 kwa lita hadi kufikia sh.1,953 kwa lita. Vinywaji vikali
ushuru umeongezeka kutoka sh.2,631 kwa lita hadi sh. 2,894 kwa lita ikiwa ni ongezeko
la sh. 263.
Waziri alisema ongezeko jingine la ushuru ni kwa bidhaa ya sigara
zisizo na vichungi zinazotengenezwa kutokana na Tumbaku inayozalishwa hapa nchini
kwa kiwango cha angalau asilimia 75% kutoka sh.9,031 hadi Sh.11,289 kwa sigara 1000.
Alisema kwa upande wa sigara zinzotengenezwa hapa nchini kwa kiwango cha angalau asilimia
75% ushuru umeongezeka kutoka sh.21,351 hadi sh.26,689 kwa sigara 1,000.
Saada
alisema sigara nyingine zenye sifa tofauti na hizo suhuru umeongezeka kutoka sh.38,628
hadi sh.48,285 kwa sigara 1,000 ikiwa ni ongezeko la sh.9,657 sawa na sh.9.65 kwa
sigara moja.
Alisema hatua hizo katika ushuru wa bidhaa kwa pamoja zinatarajiwa
kuongeza mapato ya serikali kwa kiasi cha sh. milioni 124,292. Pia Waziri huyo alisema
utaratibu wa utozaji wa kodi ya mafuta ya petrol unaotumika hivi sasa ni wa kuchelewesha
malipo ambapo kodi inakadiriwa na baada ya kukadiria malipo hufanyika katika siku
45. Alisema Tanzania ni nchi pekee inayotumia utaratibu huo katika nchi za Afrika
Masharikia ambapo utaratibu huo hutoa mwanya wa ukwepaji wa kodi na hivyo Waziri Saada
alipendekeza kuwa mara baada ya kodi kukadiriwa ilipwe mara moja.
Wakati
huo huo Serikali ya Tanzania imesema imeandaa mapendekezo ya sheria ambayo itafikishwa
bungeni ili kuangalia ni uwekezaji wa aina gani unahitaji misamaha ya kodi na ipi
haitaji. Kauli hiyo ilitolewa alhamisi tarehe 12 Juni 2014 bungeni na Waziri Mkuu
Mizengo Pinda alipokuwa akijibu swali la papo kwa papo la Murtza Mangungu (Kilwa Kaskazini-CCM).
Katika swali lake Mangungu alitaka kujua nini kauli ya serikali juu ya misamaha ya
kodi wanayopewa wawekezaji kwani sasa imekuwa ni chungu kwa viwanda vya ndani.
Pinda
alisema suala la misamaha ya kodi lilitolewa makusudi ili kuwawezesha wawekezaji kuwekeza
kwa manufaa makubwa ya nchi hapo baadae. Alisema baadhi ya wawekezaji wamekuwa wakiitumia
vyema misamaha hiyo lakini pia wapo ambao hawatumii vizuri. Alisema hata hivyo mamlaka
ya Mapato TRA na vyombo vingine vimekuwa vikifuatilia kwa karibu wawekezaji ambao
wamepata misamaha ya kodi lakini bado kuna umuhimu wa kuimarisha zaidi usimamizi.
Pinda
alisema ipo hofu kuwa misamaha hiyo inaweza kuua viwanda vya ndani kutokana na wawekezaji
kusamehewa kodi kwa muda mrefu huku wakizalisha bidhaa ambazo zinazalishwa hapa nchini.
Pinda alisema serikali imeliona hilo na kwa sasa inaendelea kulidhibiti ikiwemo kuimarisha
viwanda vya ndani ikiwemo vya ngozi, sukari na bidhaa nyingine.
“Misamaha
katika viwanda kama vya sukari, saruji vya kutoka nje ni vyema ikafutwa ili kuvipa
viwanda vyetu nguvu zaidi’’ alisema “Haiwezekani tuwe tunanunua kanga kila wakati
toka nje dawa ni kupiga ushuru mkubwa ili viwanda vyetu navyo vifanye vizuri hilo
nalo tunaliangalia.’’ Alisema heshima ya nchi yeyote Duniani ni kuwa na viwanda vyake
yenyewe na si kutegemea viwanda vya nje. Aidha Pinda alisema Wizara ya Kazi na Ajira
pamoja na Uhamiaji wametakiwa kutoruhusu ajira za wageni ambazo watanzania wanaweza
kuzifanya.
Pinda alisema Serikali imekuwa macho katika kukataza wageni toka
nje kuja kufanya kazi nchini ambazo watanzania wanaweza kuzifanya kwani kwa kufanya
hivyo ni kuwanyima fursa wazawa.
Alisema pale aina ya uwekezaji unapohitaji
wafanyakazi kutoka nje basi wataruhusiwa kufanya hivyo lakini ni lazima watanzania
kiasi fulani wawepo. ‘’Nilikwenda pale Mtwara Dangote niliona Yule mwekezaji akiwa
na wafanyakazi toka nje lakini wapo vijana wakitanzania wakifanya kazi huku wakijifunza
na hata katika Bomba la gesi pia wapo wachina lakini watanzania nao wapo.’’ Alisema.
Akizungumzia
kuhusiana na wageni kuja kufanya biashara ndogo ndogo nchini Waziri Mkuu alisema hali
hiyo inatokaka na kutokuwepo kwa viwanda vya kutosha hapa nchini. Alisema kutokana
na nchi kuwa mchuuzi wa kila kitu kumewafanya wafanyabiashara wengi kukimbilia Tanzania
huku wakiwemo walioruhusiwa kisheria na hata wale ambao hajaruhusiwa.
Kwa mujibu
wa Pinda ni vyema sasa kukawa na mkakata wa makusudi wa kuzalisha bidhaa mbalimbali
hapa hapa nchini ili kulinda viwanda vya ndani. Alisema katika kulinda viwanda vya
ndani ni bora kuweka kodi kubwa kwa bidhaa za nje zinazoweza kuzalishwa hapa nchini
ili kupunguza uingizaji wake. “Hata kama kuna mfanyabiashara analeta bidhaa hapa nchini
dawa ni kumbana tu ajenge kiwanda hicho hapa hapa nchini ili azalishe bidhaa zake’’
alisema.
Na wakati huo huo WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amesema si dhambi kwa
watanzania waliosomeshwa na fedha za walipa kodi kwenda kufanya kazi nje ya nchi.
Pinda aliyasema hayo alipokuwa akijibu swali la Rashid Ali Abdalah (Tumbe-CUF) aliyetaka
kujua ni kwanini serikali inaruhusu vijana waliosomeshwa kwa gharama kubwa kwenda
kufanya kazi nje ya nchi.
Alisema ni muhimu kwa vijana wa aina hiyo wakatiwa
moyo kwenda kufanya kazi nje lakini baada ya muda warejee nchini wakiwa na ujuzi zaidi.
Pinda alisema serikali imeliona tataizo hilo na kwa sasa wameendelea na sera mbalimbali
ambazo zitaweza kuwabakisha vijana hao hapa nchini badala ya kukimbilia nje ya nchi.
“Kwa kweli kinachowafanya vijana hawa kukimbilia nje ni mishahara hivyo kutokana na
sera zetu tunaangalia jinsi ya kuongeza mishahara hivyo nadhani itasaidia kuwafanya
wabaki hapa nchini.
Aidha Waziri Mkuu alisema tatizo la ajira kwa vijana waliohitimu
masomo si tatizo la Tanzania pekee bali ni tatizo linalozikumba nchi nyingi.
Alisema
kwa kupitia juhudi zinazofanywa na Chama cha Mapinduzi CCM tatizo hilo huenda likapata
ufumbuzi katika muda mfupi ujao. Alisema kwa sasa serikali imekuwa ikijitahidi kuwaajiri
wahitimu mbalimbali moja kwa moja wakiwemo walimu na watalaamu katika fani mbali mbali
za maisha. Pinda alisema sehemu nyingine ambao inaweza kuajiri wahitimu wengi ni sekta
binafsi na pia vijana kutumia fursa zilizopo ili kujiajiri. Kwa mujibu wa Pinda fursa
zingine ni ukanda wa kiuchumi wa EPZ nalo ni sehemu ya kukabiliana na tatizo la ajira.
Pia
Waziri mkuu Pinda katika kipindi hicho alisema kuwa serikali haitaruhusu Chuo Kikuu
cha UDOM kukataza wanafunzi 500 kufanya mitihani yao ya mwisho kwa kuwa hawajalipa
ada. Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyasema hayo alipokuwa akijibu swali la Haji Khatib
Kai (Micheweni-Cuf) aliyetaka kujua nini kauli ya serikali juu ya hatma ya wanafunzi
hao ambao wameambiwa hawatafanya mitihani kutokana na kutolipa ada.
“Mheshimiwa
Waziri Mkuu kuna taarifa kuwa kuna wanafunzi zaidi ya 500 wa Chuo Kikuu cha UDOM watazuiliwa
kufanya mitihani yao kutokana na kukosa ada na hawa ni watoto wa masikini nini kauli
ya serikali katika hili.’’ Alisema. Akijibu swali hilo Pinda alisema serikali haitaruhusu
vijana hao kukosa kufanya mitihani yao kutokana na ada. Alisema vijana hao wamesoma
kwa miaka mitatu hivyo suala la ada haliwezi kuwa sababu ya kupoteza muda wao wote.
“Tutajitahidi
vijana hao watafanya mitihani yao kama ilivyopangwa , sidhani kama kutakuwa na tatizo
na hawa vijana mara nyingi wakiwa na jambo huja kwangu kuniambia lakini kwa hili hili
hawajafika.’’ Alisema. Waziri Mkuu Pinda alisema serikali itaendelea kuzuia kufanyika
kwa mikutano ya hadhara katika mikoa ya Mtwara na Lindi mpaka hapo itakapojiridhisha
na hali ya usalama na utulivu katika mikoa hiyo. Waziri Mkuu alisema kwa sasa bado
wanaendelea kufutilia hali hiyo kwani hivi karibuni walishataka kutoa ruhusa kwa mkoa
wa Lindi lakini hali ilikabadilika.