Baraza la Makanisa Ulimwenguni limeendelea kuwa mstari wa mbele katika uhamasishaji
wa kuridhia mkataba wa udhibiti wa biashara ya silaha duniani ili kuokoa maisha ya
watu sehemu mbali mbali duniani.
Kuna maelfu
ya watu wanaofariki dunia kutokana na vita huko Syria na Sudan ya Kusini kutokana
na biashara haramu ya silaha inayowaingizia wahusika mamillioni ya dolla za kimarekani
kwa mwaka, lakini kwao utu, heshima na maisha ya mwanadamu hayana nafasi bali “pochi”
imepewa kipaumbele cha kwanza.
Baraza la Makanisa linaendelea kuzihamasisha
Serikali mbali mbali duniani ili kuridhia mkataba wa kimataifa utakaodhibiti biashara
ya silaha duniani, jambo ambalo si rahisi sana wanasema wachunguzi wa mambo kwani
hapa masuala ya uchumi yanapewa kipaumbele cha kwanza kuliko hata uhai wa binadamu.
Wajumbe wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni kutoka Barani Afrika wamekuwa wakitaka
mkataba wa udhibiti wa silaha kushughulikia pia silaha ndogo ndogo na risasi zinazosababisha
maafa au majeraha makubwa kwa watu. Baraza la Umoja wa Mataifa katika mkutano wake
wa hivi karibuni umepitisha mkataba wa kudhibiti biashara ya silaha unaowaingizia
wahusika faida ya dolla billioni 80 kwa mwaka, kwa kura 154 zilizounga mkono na kura
3 kutoka Syria, Korea ya Kaskazini na Iran zilipinga muswada huu!