2014-06-10 06:49:58

Mikakati mipya ya kuwahudumia Zingari


Utume wa Kanisa miongoni mwa Zingari unahitaji sera na mikakati mipya ya shughuli za kichungaji zinazotekelezwa na Mama Kanisa kwa jamii hii, ili kubomo kuta za utengano: kijamii, kisiasa na kitamaduni ndani ya Jamii. RealAudioMP3

Hivi ndivyo anavyofafanua Kardinali Antonio Maria Vegliò, Rais wa Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum wakati wa kufunga kongamano la kimataifa lililowashirikisha wajumbe kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ili kwa pamoja kupembua mikakati ya Kanisa na Zingari ili kutangaza Injili pembezoni mwa Jamii.

Lengo la kongamano hili lilikuwa ni kuchambua tena mikakati ya shughuli za kichungaji inayotekelezwa na Mama Kanisa kwa ajili ya Zingari, ili iweze kuwa na mguso na mashiko kwa wahusika kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya katika mazingira yao. Wajumbe wamepembua historia ya Zingari tangu Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, kumbu kumbu ya miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipokutana na Zingari huko Pomezia kunako tarehe 26 Septemba 1965, huu ukawa ni mwanzo wa shughuli za kichungaji kwa Zingari.

Kwa namna ya pekee, wajumbe wameangalia changamoto za kichungaji zinazotolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa kichungaji, Injili ya Furaha, Evangelii gaudium. Wajumbe wamegusia matatizo, changamoto na fursa ambazo zinawafanya Zingari wakati mwingine kutengwa na jamii wanamoishi hasa katika masuala ya afya na tiba; makazi, fursa za ajira na elimu.

Kuna mikakati inayoendelea kufanyiwa kazi ili kuwawezesha watoto wa Zingari kwenda shule, umuhimu wa kuzingatia utawala wa sheria na amani kati ya jamii husika. Makanisa mahalia yanaendelea kuhimizwa kuweka mikakati ya kichungaji kifamilia na kirika ili kuwawezesha Zingari kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa.

Utamadunisho wa imani katika mazingira wanamoishi Zingari ni kati ya changamoto zilizoainishwa na wajumbe wakati wa mkutano wao uliohitimishwa mjini Vatican. Ni matumaini ya wajumbe hawa kwamba, Watumishi wa Mungu Emilia Fernàndes na Juan Ramòn Gil, Mashahidi wa Kizingari wataweza kutangazwa kuwa Wenyeheri na Mama Kanisa.

Kumbu kumbu ya miaka 50 tangu Papa Paulo VI alipowatembelea Zingari Pomezia ni tukio muhimu sana katika mikakati ya kichungaji inayotekelezwa na Kanisa tangu wakati huo, kwani Zingari wanaweza kukutana na ndugu na jamaa wanaopenda kama alivyopenda Yesu mwenyewe! Hivi ndivyo Baba Mtakatifu Francisko alivyokazia wakati alipokutana na Wajumbe wa kongamano la kimataifa kuhusu utume wa Kanisa miongoni mwa Zingari sehemu mbali mbali za dunia.

Imetayarishwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.