2014-06-10 10:48:20

Kombe la Dunia Brazil na kasheshe zake!


Mashindano ya Kombe Dunia kwa Mwaka 2014 yanaanza kutimua vumbi kwenye viwanja kumi na viwili kutoka Rio hadi Manaus nchini Brazil. Hiki kitakuwa ni kipindi cha kusuka na kunyoa. Mtawasikia mashabiki wa mpira wa miguu wakishangilia na kulilia timu zao za kitaifa! Ni mambo ya kawaida!

Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil kwa kushirikiana na wadau mbali mbali wametoa kanuni kumi zinazolenga kuisaidia Brazil ili kujenga usawa na haki kwa wote. Jambo la msingi kwa Serikali ni kuhakikisha kwamba, inatoa fursa za ajira bora kwa wote; watu wapewe nafasi ya kuhitimu masomo, uhakiki wa demokrasia kwa njia ya haki; wananchi wa Brazil wanasubiri kuona mabadiliko katika sekta ya kilimo na uzalishaji; ulinzi na usalama kwa vijana na watoto; udumishaji wa utamaduni wa tofauti miongoni mwao.

Serikali haina budi kujifunga kibwebwe kuhakikisha kwamba inapambana kufa na kupona na vitendo vya rushwa, wizi naufisadi kwa kujikita katika ukweli na uwazi; Serikali haina budi kujielekeza zaidi katika maboresho ya masuala ya kijamii kwa kukazia afya kwa wote.

Kwa njia hii, Serikali ya Brazil itakuwa inajibu changamoto kubwa ambazo zimekuwa zikijitokeza nchini humo kutokana na gharama kubwa za kuandaa mashindano ya Kombe la Dunia kwa Mwaka 2014 yanayoanza kutimua vumbi nchini Brazil kuanzia tarehe 12 Juni 2014.








All the contents on this site are copyrighted ©.