Ifuatayo ni hotuba iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania wakati wa ufunguzi
wa huduma za uchunguzi wa Saratani ya mlango wa kizazi nay a matiti mkoani Tabora,
tarehe 7 Juni 2014.
Niruhusuni nianze kwa kuwashukuru Waziri wa Afya na Ustawi
wa Jamii, Dkt. Seif Rashid (aliyewakilishwa hapa leo na Naibu Waziri Mhe.Dkt. Stephen
Kebwe) na Mwenyekiti wa Chama cha Madakatari Wanawake Tanzania (MEWATA), Dkt. Sarafina
Mkuwa kwa kunialika kuja kuzindua huduma za uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi
na saratani ya matiti Mkoani Tabora. Nawapongeza nyote kwa maandalizi mazuri kwani
ni ukweli usiopingika kuwa shughuli hii imefana sana. Aidha, nawashukuru wenyeji wetu
wa Mkoa wa Tabora wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa, Mheshimiwa Fatma Mwasa, kwa mapokezi
mazuri mliyonipatia mimi, mke wangu na wageni wenzetu. Sikutegemea kupata mapokezi
tofauti na haya hapa Tabora, kwani upendo wenu kwangu na ukarimu wenu tunaujua na
unasifika na wengi.
Madhumuni ya Ziara Ndugu Wananchi;
Nimekubali
kuja kujumuika nanyi katika uzinduzi huu, siku ya leo, ili kuongeza sauti yangu na
uzito kuhusu shughuli hii muhimu na adhimu inayofanywa na Madaktari Wanawake hapa
nchini. Ni ukweli ulio wazi kuwa MEWATA imesaidia kuokoa maisha ya akinamama wengi
nchini ambao, vinginevyo, wangepoteza uhai kwa saratani hizi mbili zinazowapata wanawake.
Hatuna budi kuvunja ukimya na kuungana na Madaktari Wanawake kuzungumzia maradhi haya
na kuelimishana ili wananchi, wadau na Serikali kwa umoja wetu au mmoja mmoja, tuchukue
hatua stahiki za kukabiliana na maradhi haya.
Aidha, ni nafasi nzuri ya kutoa
pongezi zangu kwa wanachama wa MEWATA kwa kazi kubwa na nzuri waifanyayo na mafanikio
yaliyopatikana. Sijui hali ya maradhi haya ingekuwaje hapa nchini kama Madaktari Wanawake
wasingeamua kufanya kazi hii njema wanayoifanya. Kwa niaba ya wanawake na wanaume
wote wa Tanzania tafadhali pokeeni pongezi zetu za dhati. Endeleeni kufanya kazi hii
njema na Mwenyezi Mungu atawalipa kwa wema wenu na mioyo yenu ya huruma. Nawaahidi
kuendelea kuwaunga mkono kwa hali na mali na kwa kadri ya uwezo utakavyoniruhusu.
Nimefurahi
sana kwamba ndugu zetu wa MEWATA wameweza kufika hapa Tabora siku ya leo. Mtakumbuka
kuwa nilipokuja kwenye Sherehe za Siku ya Wanawake Duniani tarehe 8 Machi, 2010, niliahidi
kwamba nitawaomba MEWATA waje kufanya uchunguzi wa saratani za mlango wa kizazi na
matiti kwa akinamama. Hayawi hayawi leo yamekuwa. Nawashukuru sana viongozi na wanachama
wa MEWATA kwa kuja kwenu. Mmenitoa kimasomaso. Wahenga walisema: “Ada ya Mja kunena,
muungwana na vitendo”. Ndugu zangu wa Tabora ahadi imetimia, kazi kwenu. Jitokezeni
kwa wingi kupima muokoe maisha yenu.
Hali ya Magonjwa ya Saratani ya Wanawake
Nchini
Ndugu Wananchi,
Tanzania inatambulika kuwa ni moja ya nchi
zenye kiwango kikubwa cha maradhi ya saratani ya mlango wa kizazi hapa Afrika ya Mashariki.
Inakadiriwa kuwa takriban wanawake 56 katika kila wanawake 100,000 hupata saratani
hii. Inakadiriwa pia kuwa zaidi ya watu 35,000wanapata saratani hii kila mwaka na
zaidi ya watu 27,000 hupoteza maisha. Mwaka 2010 peke yake, wanawake wapatao 6,000
waligundulika kuwa na saratani ya mlango wa kizazi na wanawake 4,000kati yao walifariki
dunia.
Wataalamu wanatuambia kuwa, saratani hii huwapata wanawake wa umri
wa miaka 30 na 50. Aidha, wanawake wanaoishi na virusi vya UKIMWI wako katika hatari
zaidi ya kupata ugonjwa huo kwa asilimia 50. Pamoja na tatizo hili, bado tunayo changamoto
ya saratani ya matiti ambayo ni ya pili kwa kusababisha vifo vya wanawake wengi nchini.
Hivyo basi, hapa nchini wanawake wako kwenye hatari kubwa ya kufa kwa saratani kuliko
wanaume kwa sababu saratani nyinginezo, hazibagui ukiacha ile ya tezidume inayowapata
wanaume pekee.
Hatua za Tahadhari za Kuzingatiwa
Bahati nzuri,
saratani ya mlango wa kizazi na saratani ya matiti zinaweza kutibika ikiwa zitagunduliwa
mapema. Njia pekee ya kuweza kugundua mapema ni kupima mara kwa mara. Wataalamu wanashauri
kuwa ni vyema wanawake wenye umri wa kati ya miaka 30 na 50 wakachunguza afya zao
walau mara moja katika kila miaka mitatu. Na, kwa wanawake wanaoishi na virusi vya
UKIMWI wanashauriwa kuchunguzwa walau mara moja kwa mwaka.
Bahati mbaya sana,
uzoefu umeonyesha kuwa wanawake wengi hufika hospitali wakati ambapo ugonjwa umeshapea
na kuenea sehemu nyingine za mwili. Wanakwenda hospitali wakati maradhi yamefikia
hatua isiyoweza kutibika na hivyo kupoteza maisha. Hivyo basi, kupima na kugundulika
mapema kwa saratani ni hatua muhimu sana ya kuepusha vifo vinavyotokana na maradhi
hayo. Bahati nzuri hivi karibuni kumekuwepo na mwamko na mwitikio mzuri wa kujitokeza
kwa wanawake wengi kupima saratani ya matiti. Haya ni matunda ya kazi nzuri inayofanywa
na MEWATA. Juhudi hizi zinapaswa kuendelezwa. Zinastahili kuungwa mkono.
Hatua
Zinazochukuliwa na Serikali Ndugu Wananchi;
Serikali imechukua hatua
mbalimbali katika kukabiliana na saratani ya mlango wa kizazi. Wizara ya Afya na Ustawi
wa Jamii imeanzisha Programu inayoshughulikia masuala ya Saratani za Uzazi katika
Kitengo cha Afya ya Uzazi na Mtoto mwaka 2008. Kupitia programu hii tuna Mpango Mkakati
wa Kukinga na Kudhibiti Saratani ya Mlango wa Kizazi (2011-2016). Mwongozo wa kutoa
huduma umeandaliwa pamoja na miongozo ya mafunzo kwa watoa huduma na ujumbe wa kuelimisha
jamii kupitia njia mbalimbali. Kupitia programu hii tumeweza kuanzisha vituo zaidi
ya 130 vinavyotoa huduma ya uchunguzi wa Saratani ya Mlango wa Kizazi katika Mikoa
17 hapa nchini. Ukilinganisha na mwaka 2008 tulipokuwa na vituo vinne tu vilivyokuwa
vinatoa huduma hii ya uchunguzi wa Saratani ya Mlango wa Kizazi na tiba ya mabadiliko
ya awali, haya ni maendeleo makubwa.
Ndugu Wananchi, Kupitia Wizara ya Afya
na Ustawi wa Jamii, Serikali imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo
MEWATA, Marie Stopes, WAMA na wengineo kutekeleza mpango wa “Utepe wa Pinki na Utepe
Mwekundu” yaani “Pink Ribbon Red Ribbon”. Kupitia program hiyo, kampeni ya uchunguzi
wa saratani ya mlango wa kizazi na matiti ilizinduliwa katika mkoa wa Mwanza mwezi
Machi mwaka huu katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani.
Kupitia mpango
huo, tumekabidhi mashine 16 za kutolea huduma za matibabu ya mabadiliko ya awali ya
saratani ya mlango wa kizazi (Cryotherapy machine) kwa mikoa ya Mwanza, Mara, Iringa,
Njombe na Mbeya. Mipango inaendelea kwa mikoa iliyosalia pamoja na Tabora kupatiwa
mashine hizo kuendeleza juhudi za Serikali kupanua upatikanaji wa huduma hizi katika
mikoa yote nchini.
Lengo letu katika kufanya hivyo ni kutaka kupunguza mzigo
mkubwa unaoielemea Hospitali yetu ya kuu kansa ya Ocean Road. Pia, tunataka kuwapunguzia
wanawake adha na gharama ya kusafiri umbali mrefu hadi Dar es Salaam kwa ajili ya
uchunguzi. Tunatambua umuhimu wa huduma hizi kuwa karibu zaidi na walipo watu ili
ziwafikie wanawake wote bila kujali hali zao za kipato.
Ndugu Wananchi;
Katika
jitihada za kutokomeza maradhi haya, Serikali, kupitia Mpango wa Taifa wa Chanjo,
imeanza kutoa chanjo ya kuzuia Saratani ya mlango wa Kizazi ya “Human Papilloma Virus
(HPV)”. Chanjo hii hutolewa kwa watoto wa kike wenye umri wa miaka 9. Chanjo hii hukinga
wasipate maambukizi ya virusi ambavyo husababisha Saratani ya Mlango wa Kizazi. Wizara
ya Afya tayari imezindua mpango huo wa utoaji wa chanjo ya HPV kwa wasichana tarehe
29 Aprili, 2014 wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Chanjo Duniani na mama Salma Kikwete.
Mpango huo ulizinduliwa kwa Halmashauri tano za Hai, Siha, Moshi Vijijini, Moshi Mjini
na Rombo za Mkoa wa Kilimanjaro, kuashiria kuanza kwa utekelezaji wa azma ya kutoa
chanjo hii nchi nzima ifikapo mwaka 2016.
Ndugu Wananchi;
Napenda kutoa
pongezi na shukrani za pekee kwa MEWATA kwa kazi nzuri na kubwa ya kukuza uelewa wa
jamii na kuhamasisha uchunguzi wa saratani zinazowapata wanawake. Ni dhahiri kwamba
ili jambo hili lifanikiwe lazima liwe na mshika bango wake. Bahati nzuri ndugu zetu
wa MEWATA wamejitoa kimasomaso na wamefanya kazi ya Serikali kuwa rahisi. MEWATA imekuwa
inafanya kazi kwa karibu na Serikali pamoja na wadau wengine katika kuhamasisha jamii
kuhusu masuala ya Saratani ya Matiti na ya Mlango wa Kizazi. Kama nilivyokwisha kusema
awali, juhudi hizo zimewafikia wanawake wengi nchini na kuokoa maisha yao.
Aidha,
napenda kuchukua fursa hii kutambua na kutoa shukrani maalum kwa Shirika la Marie
Stopes na wadau wote ambao wanashirikiana na Serikali katika kupambana na tatizo hili
kubwa la Saratani ya Mlango wa Kizazi. Vilevile, tunawashukuru wale wote wanaotoa
huduma ya afya ya uzazi na mtoto nchini. Napenda kwa mara nyingine tena kuwahakikishia
ushirikiano wa Serikali ya CCM ninayoiongoza kwenu. Ni, dhamira yetu kupunguza na
ikiwezekana hata kumaliza kabisa vifo vitokanavyo na Saratani ya Mlango wa Uzazi na
Saratani ya Matiti ambazo kwa kweli zinaweza kuzuilika.
Wito kwa Wananchi
Ndugu
Wananchi;
Natoa wito kwa wanawake wa Tabora kujitokeza kwa wingi kufanyiwa
uchunguzi wa saratani hizi na wataalamu walioko hapa. Napenda kuwatoa hofu kuwa saratani
ya mlango wa kizazi na saratani ya matiti siyo magonjwa ya aibu au ya mkosi au uchawi
au laana na wala siyo magonjwa yasiyotibika. Magonjwa haya huweza kumpata mwanamke
ye yote, awe ameolewa au hajaolewa, awe amezaa au hajazaa, awe tajiri au maskini.
Madhali ni mwanamke anaweza kupata. Sharti lake la kupona ni kugundulika mapema na
kuanza tiba mapema.
Kuchelewa kugundulika na kuchelewa kuanza matibabu ndiko
kunakosababisha vifo kutokana na maradhi haya. Waswahili wana msemo usemao, mficha
maradhi kifo humuumbua. Hivyo ndugu zangu kina mama nashauri mfanye uchunguzi mapema,
ili kama kuna tatizo muanze tiba mapema.
Napenda kutumia fursa hii, kuwaasa
akina baba na walezi nao kusaidia katika juhudi za kuzuia na kutibu magonjwa haya
ya saratani ya wanawake. Mwanamke anayepata magonjwa haya anahitaji matunzo na upendo
siyo masimango na unyanyapaa. Masimango na unyanyapaa huwafanya wanawake waogope kujitokeza
kuchunguza afya zao na kupatiwa tiba kwa kuogopa kubaguliwa au kuachwa. Magonjwa haya
yanatibika. Si kila mwanamke anayepata saratani hufariki dunia. Kinachotakiwa ni baba
na mama kushirikiana kumpeleka mama kufanyiwa uchunguzi na kupata tiba iwapo atagundulika
kuwa na maradhi. Saratani siyo ugonjwa wa zinaa, hivyo, msiwanyanyapae akina mama
bali muwalee na kuwatunza ili waweze kurejea katika hali zao za kawaida. Akina baba
muwe ndiyo nguzo ya mafanikio katika mapambano dhidi ya saratani.
Na, kwa wanaume
wenzangu, tujenge mazoea ya kupima afya zetu hususan kuhusu saratani ya tezidume (prostate).
Hii ni saratani inayoua wanaume wengi duniani na hapa nchini. Lakini nayo kama zilivyo
saratani za matiti na mlango wa kizazi zinatibika kama zitagundulika mapema. Kila
mkienda kupima afya pimeni afya ya tezidume mjue mustakabali wenu.
Ndugu Wananchi;
Sote
tukiungana pamoja tunaweza kutokomeza saratani ya mlango wa kizazi na saratani ya
matiti. Nia ya kutokomeza maradhi haya tunayo, sababu ya kutokomeza tunayo na uwezo
wa kuyatokomeza tunao. Kinachotakiwa ni kuunganisha nguvu zetu pamoja. Mimi na mke
wangu Mama Salma Kikwete tuko nanyi na tutaendelea kuwa nanyi bega kwa bega katika
vita hii sasa na hata baada ya kuacha Urais mwakani. Inawezekana, timiza wajibu wako!
Ndugu
Wananchi;
Kwa vile niko Tabora ni vyema nikatumia nafasi hii pia, kuyazungumzia
baadhi ya mambo niliyoyazungumzia au kuahidi kufanya safari zilizopita. Kwa upande
wa barabara, napenda kuwahakikishia kuwa barabara kuu zinazoendelea kujengwa hapa
Mkoani Tabora tutazimaliza. Subira yavuta heri. Barabara ya Urambo –Kaliua ujenzi
utaanza mwaka huu wa fedha na Chaya – Nyahua, mchakato wa kutafuta fedha unaendelea
ili nayo ujenzi wake uweze kuanza kabla ya mimi kumaliza kipindi changu cha uongozi.
Kuhusu kupata maji ya Ziwa Victoria, kwa Igunga, Nzega, Tabora, Urambo na Sikonge
hatua za awali zimeanza na kinachofuatia ni kutafuta fedha kwa ajili ya mradi huo
mkubwa. Tunakusudia kuiomba Serikali ya India ambayo ndiyo iliyogharamia matayarisho
ya mradi. Tuna matumaini ya kufanikiwa. Sote tuzidi kuomba iwe hivyo.
Kwa upande
wa tatizo la wakulima wa tumbaku kutokulipwa stahili zao na vyama vya ushirika nimeelezwa
na kulielewa. Kuna tuhuma za wizi na ubadhilifu. Nimemuagiza Inspekta Jenerali wa
Polisi atume watu wake wa upelelezi wa makosa ya Jinai waje wafanye uchunguzi ili
wahusika wakamatwe na kufikishwa Mahakamani na kupewa adhabu zinazostahili. Ameniahidi
kuwa keshokutwa Jumatatu watu hao watakuja. Wapeni ushirikiano unaostahili ili tukomeshe
uhalifu na dhuluma zinazofanywa na Maofisa wa Vyama vya Ushirika na taasisi za fedha
kwa muda mrefu sasa.
Baada ya kusema hayo, naomba nitangaze sasa zoezi hili
la uchunguzi wa Saratani ya Mlango wa Kizazi na ya Matiti limefunguliwa rasmi.