Haki ya kweli inajikita katika mchakato unaolenga kusahihisha, kuboresha na kuelimisha
makosa yaliyojitokeza badala ya kulaani na kuhukumu! Hivi ndivyo Baba Mtakatifu Francisko
anatahadharisha wajumbe wa wanaoshiriki kongamano la kumi na sita kimataifa la wanasheria
kutoka Amerika ya Kusini sanjari na kongamano la tatu la sheria kimataifa.
Ni
matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, sheria inaheshimu na kuzingatia utu
wa mwanadamu na haki zake msingi pasi na ubaguzi pamoja na kuhakikisha kuwa, wanyonge
ndani ya jamii wanalindwa zaidi.
Baba Mtakatifu anasikitika kusema kwamba,
magereza Amerika ya Kusini yamefurika kwa wafungwa, hali ambayo inawanyanyasa na kuwadhalilisha
wafungwa ambao wanahukumiwa adhabu mbili kwa mpigo! Kuna haja ya jamii kutambua kwamba,
wakati mwingine kinzani na mapambano ya kijamii ni matokeo ya ukosefu wa haki na usawa
katika masuala ya kiuchumi na kijamii, hali ambayo inawafanya baadhi ya watu kujichukulia
sheria mikononi mwao.
Adhabu kali bado hazijafanikiwa kupunguza vitendo vya
uhalifu na makosa ya jinai katika jamii nyingi. Hapa kuna haja ya kupambanua kati
ya haki na mchezo wa kulipizana kisasi, kwa kuangalia uwezekano wa mfungwa kujirekebisha
na kuanza upya hija ya maisha yake ndani ya jamii.