2014-06-08 11:55:51

Waamini walei ni tunda la Pasaka na Pentekoste!


Askofu mkuu Yuda Thaddeus Ruwaichi wa Jimbo kuu la Mwanza, Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, Waamini walei, Wakleri na Watawa kwa pamoja wanaunda Taifa la Mungu. RealAudioMP3

Mtaguso mkuu wa Pili wa vatican unabainisha nafasi, utume, karama na mchango maalum wa waamini walei katika maisha na utume wa Kanisa ulimwenguni. Kuna majimbo ambayo yamepiga hatua kubwa kwa waamini walei kuelewa wito na maisha yao ndani ya Kanisa na kwamba, wanajitahidi kuuishi Ukristo wao kikamilifu.

Waamini walei wanaoishi kikamilifu Ukristo wao wanatekeleza karama ya Pentekoste, siku ambayo Roho Mtakatifu alilishukia Kanisa na kutia nguvu ya kumshuhudia Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Ushuhuda wa waamini walei ni tunda la mshikamano wao wa ubatizo na Kristo mfufuka. Wao ni watoto wa Pasaka na Penteskote.

Askofu mkuu Ruwaichi anasema kwamba, Kanisa linapoajiandaa kwa ajili ya maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, iwe ni fursa ya kuangalia pia mapungufu yanayojitokeza katika maisha ya waamini walei kiasi hata cha kushindwa kutekeleza dhamana na wajibu wao ndani ya Kanisa. Wakleri wajichunguze na kuangalia pale ambapo wamekuwa ni kikwazo kwa ustawi na maendeleo ya waamini walei ndani ya Kanisa, kiasi kwamba, wanashindwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa ujenzi wa Fumbo la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa, ili kurekebisha kasoro hizi na kuanza kuwashirikisha waamini walei kikamilifu, kila upande ukitambua na kuheshimu karama na dhamana yake ndani ya Kanisa.







All the contents on this site are copyrighted ©.