2014-06-08 14:39:05

Mshangao ndio zawadi kubwa ya Pentekoste!


Mara baada ya maadhimisho ya Ekaristi Takatifu katika Sherehe ya Pentekoste, Jumapili tarehe 8 Juni 2014 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Wakati wa Sala ya Malkia wa Mbingu, Baba Mtakatifu anasema kwamba, Pentekoste inafunga kipindi cha Pasaka kwa mshangao mkubwa, kwa Roho Mtakatifu kuwashukia Mitume, kiasi kwamba, wanapata ujasiri na nguvu ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu inayoeleweka na wote! Mahali ambapo Roho Mtakatifu anafika, kunabadilika na huu ndio mwanzo wa Kanisa linalojidhihirisha hadharani, ni Kanisa linaloshangaza na kuonesha "vurugu".

Pentekoste anasema Baba Mtakatifu ni Sherehe ya kushangaza, kwani hakuna mtu aliyekuwa anategemea jambo lolote kutoka kwa mitume baada ya kifo cha Kristo, ni watu waliobaki kama watoto yatima, Pentekoste inawashangaza wengi kwani kila mtu aliweza kusikia Habari Njema ikitangazwa kwa lugha yake mwenyewe, matendo makuu ya Mungu.

Kanisa lililozaliwa wakati wa Pentekoste linazua mshangao kwani linaanzishwa kwa nguvu ya Mungu na kutangaza Ufufuko wa Kristo kwa lugha ya upendo. Mitume wamejazwa nguvu ya Roho Mtakatifu na wanazungumza kwa ujasiri na ukweli kadiri ya Roho Mtakatifu. Hivi ndivyo Kanisa linavyopaswa kuwa na nguvu ya kutangaza Kristo aliyeshinda kifo na kwamba, Mwenyezi Mungu kwa njia ya uvumilivu yuko tayari kuwaponya na kuwasamehe, utume ambao Yesu amelikabidhi Kanisa lake.

Baadhi ya watu mjini Yerusalemu walitaka kuwaona mitume wa Yesu wakiwa wamejifungia ndani bila kusababisha vurugu kama zile zilizojitokeza wakati wa Pentekoste, lakini Yesu anawatuma ulimwenguni kutangaza Habari Njema ya Wokovu. Hili ni Kanisa ambalo liko kwa sababu linatumwa kukutana na watu ili kuwatangazia Habari Njema ya Wokovu hata kama Habari hii itahangaisha dhamiri za watu. Ni Kanisa linalokumbatia ulimwengu bila kumezwa.

Bikira Maria alikuwepo siku ile ya Pentekoste akiwa anasali na Mitume wa yesu. Ndani mwake, Roho Mtakatifu ametenda mambo makuu, kwa kumwezesha kuwa ni Mama wa Mkombozi na Mama wa Kanisa.

Mara baada ya Sala ya Malkia wa Mbingu, Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaoungana nao, yaani Papa Francisko, Patriaki Bartolomeo wa kwanza na Marais kutoka Israeli na Palestina kwa ajili ya kuombea amani huko Mashariki ya Kati.







All the contents on this site are copyrighted ©.