2014-06-08 08:52:27

Kapteni Francisko akazia: shule, kazi na michezo!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi jioni tarehe 7 Juni 2014 ameshiriki katika maadhimisho ya miaka 70 ya Chama cha Michezo Italia CONI kwa kukutana na kuzungumza na umati wa vijana waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro pamoja na viunga vyake.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, anatambua umuhimu wa michezo kama mang'amuzi ya malezi, jambo linalowahusisha wadau wote wa michezo. Hii ni njia muhimu sana katika malezi na majiundo ya watoto na vijana, katika mwelekeo wa kujitafutia kazi, kujitegemea na kuwa makini katika maadili na utu wema, bila kuwa "mateja" wa dawa za kulevya wala ulevi wa kupindukia.

Shule, michezo na kazi ni mambo muhimu sana katika maisha ya ujana kwa ajili ya afya ya roho na mwili. Michezo iwasaidie vijana kutafuta mafao ya wengi ndani ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake; michezo iwawezeshe vijana kukutana na Mwenyezi Mungu ili kupata taji lisiloharibika kamwe! Michezo ni shule ya ukarimu inayowajengea watu huweza wa kuwafungulia wengine milango ya maisha yao, lakini zaidi kwa wale ambao hawakubahatika katika jamii, ili nao waweze kushirikisha karama na vipaji vyao!

Michezo ni dhamana inayowajibisha na kuchosha, lakini inamwezesha mchezaji kupata haki, uzuri na kushirikiana na wengine ili kuondokana na upweke hasi, ubinafsi na uchoyo katika maisha. Michezo ni fursa ya kukutana na kusaidiana katika maisha, kwa kuheshimiana na kukua pamoja kama ndugu. Ni mahali pa kukuza na kuimarisha miito mitakatifu ya maisha ya kipadre na kitawa, ndiyo maana michezo Parokiani ni jambo linalopaswa kupewa kipaumbele cha pekee kadiri ya maisha na utume wa Kanisa. Michezo ni chachu ya umissionari ndani ya Kanisa, inayowawezesha watu kukutana na Yesu Kristo!

Baba Mtakatifu anawashukuru wanamichezo kwa kumteuwa kuwa ni Kapteni wao, changamoto ya kushikamana ili kujenga na kuimarisha umoja kama timu na kwamba, mchezo mkubwa ulioko mbele yao ni kutangaza Injili ya Furaha kwa watu wa mataifa. Kila mwanamichezo ashirikishe kipaji na karama yake kama alivyohimiza Yesu kwa wafuasi wake, ili kuwashirikisha wengine matumaini na imani. Kwa wanamichezo wanaojikita katika shule, kazi na michezo, kwani matumizi haramu ya dawa za kulevya au ulevi wa kupindukia hauna nafasi kamwe.

Mwishoni, Baba Mtakatifu amewatakia kheri na baraka katika maadhimisho ya Siku kuu ya Pentekoste na amewaomba wazidi kumwombea ili aendelee kutekeleza dhamana na wajibu wake kadiri ya mapenzi ya Mungu hadi pale Mwenyezi Mungu atakapomwita kwenye makao ya uzima wa milele.

Siku hii imefunikwa kwa michezo mbali mbali iliyofanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican pamoja na viunga vyake. Wanamichezo walipata fursa ya kushiriki pia Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia







All the contents on this site are copyrighted ©.