2014-06-07 07:14:41

Vyama vya kitume ni matunda ya Roho Mtakatifu!


Baraza la Maaskofu Katoliki Canada katika maadhimisho ya Siku kuu ya Pentekoste linasema kwamba, vyama mbali mbali vya kitume vinavyotekeleza dhamana yake ndani ya Kanisa Katoliki ni alama na kielelezo cha nguvu ya Roho Mtakatifu katika ulimwengu mamboleo.

Kila mwanachama wa chama na mashirika ya kazi za kitume anapaswa kutolea ushuhuda wa imani yake kwa njia ya matendo kama sehemu ya mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu. Imani hii tendaji inaweza kutekelezwa hata katika hali ya ukimya pasi na makeke, lakini inakuwa ni chachu katika kuyatakatifuza malimwengu, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linakazia kwa namna ya pekee kabisa neema ya kushikamana ili kujenga umoja na udugu, waamini wote wakitambuana kuwa ni kaka na dada katika Kristo, kwani Roho Mtakatifu anawaongoza wote kuelekea katika umoja na mshikamano katika mambo matakatifu. Roho Mtakatifu ni mdau mkuu wa Uinjilishaji, changamoto ya kujitosa kimasomaso kuwaendea maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kutokana na utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Vyama na mashirika ya kitume yajipambanue kwa kutafuta uzuri, ukweli pamoja na kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha yao. Karam ana mapaji ya Roho Mtakatifu yatumike kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa na Jamii inayowazunguka. Ni wajibu wa kila chama na shirika la kitume kupyaisha na kumwilisha karama yake katika uhalisia wa maisha ya watu wanaowazunguka, ili kweli Injili ya Furaha iweze kuwagusa na kufahamika na watu wengi zaidi!








All the contents on this site are copyrighted ©.