Baba Mtakatifu Francisko anasema umefika wakati wa kubomoa kuta zinazowatenganisha
watu na badala yake kujenga madaraja yanayowaunganisha watu na hivyo kujisikia kuwa
ni ndugu wamoja hata katika tofauti zao za kimsingi. Umefika wakati wa kuondokana
na falsafa ya kinzani na kichongo na badala yake kujenga amani, utulivu na umoja wa
kweli!
Sherehe ya Pentekoste kwa Mwaka 2014 itakuwa na umuhimu wa pekee pale
ambapo Baba Mtakatifu Francisko ataungana na Rais Shimon Peres wa Israel na Rais Mahamoud
Abbas wa Palestina kumwomba Mungu wa amani aweze kuwajalia wananchi wanaoishi Mashariki
ya Kati kupata amani ya kudumu. Sala hii inatarajiwa kufanyika kwenye Bustani za Vatican
majira ya jioni.
Hii si sala ya majadiliano ya kidini, bali ni kipindi cha
kukaa na kutafakari kwa pamoja wote wakimwelekea Mwenyezi Mungu kuomba amani kwa kutambua
kwamba, amani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi mungu inayomwajibisha pia mwanadamu. Baba
Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa watu wa amani katika
sala na matendo.
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa watumiaji
wa mitandao ya kijamii anasema kwamba, sala inaweza yote! Anawaalika watu kusali kwa
ajili ya kuombea amani Mashariki ya Kati pamoja na sehemu mbali mbali duniani.