2014-06-06 08:44:36

Upadre ni huduma!


Seminari ni mahali ambapo majandokasisi wanafundwa kiroho, kiakili, kiutu, kimaadili na kitamaduni kwa kutambua kwamba, wanahimizwa kuwa karibu zaidi na Kristo katika maisha na utume wao kwa njia ya Sala, Sakramenti na tafakari ya kina ya Neno la Mungu. RealAudioMP3

Katika majiundo yao ya awali na endelevu majandokasisi watambue kwamba, wanaitwa kumfuasa Kristo kwa karibu zaidi na kwamba, wako huru kuitikia wito huo na kuanza kuambatana na Yesu, au kuukataa na kuendelea na mipango mingine ya maisha.

Kwa jandokasisi anayekubali mwito wa kumfuasa Kristo kama Padre anapaswa kutambua anachangamotishwa kuonesha ile taswira ya Yesu mchungaji mwema anayejisadaka kwa ajili ya huduma, ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo. Hii ndiyo changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu wakati wa ziara yake ya kikazi nchini Cameroon kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 100 ya Ukristo Jimbo kuu la Bamenda, kwenye Seminari kuu ya Nkolbisson, Jimbo kuu la Yaoundè, Cameroon. Seminari hii ina majando kasisi 120 wanaojiandaa kwa ajili ya wito na maisha ya kipadre.

Kardinali Filoni amewataka waseminari katika majiundo yao ya Kikasisi kuwa kweli ni mashahidi wa Injili ya Furaha kama anavyohimiza Baba Mtakatifu Francisko; vyombo muhimu katika utekelezaji wa kazi ya ukombozi iliyoanzishwa na Yesu Kristo mwenyewe. Wao wanapaswa kuwa ni Kristo mwingine, “Alter Christus”, mabalozi waaminifu na wa kweli kati ya watu, wanaoshiriki katika mchakato wa mabadiliko ya maisha yanayopaswa kuanzia kwa majandokasisi wenyewe!

Majandokasisi wajifananishe na Kristo katika kila ngazi ya maisha yao: kibinadamu, kiakili, kiroho na katika masuala ya kichungaji. Mambo haya yanatekelezeka kwa njia ya sala ya kijumuiya na sala binafsi, Yesu daima akiwa ni dira na mwelekeo wa maisha. Majiundo haya yanaboreshwa na kurutubishwa kwa njia ya Sakramenti za Kanisa hasa Sakramenti ya Ekaristi Takatifu pamoja na Sakramenti ya Upatanisho inaymwonjesha mwamini upendo na huruma ya Mungu isiyokuwa na kifani. Tunu hizi muhimu katika majiundo ya kikasisi, zitawawezesha kweli kuwa ni wachungaji wanaopeta katika upendo na huduma kwa Familia ya Mungu.

Ili kweli majandokasisi waweze kuwa ni mashahidi wa wa Injili ya Furaha hawana budi kuachana kabisa na tabia ya unafiki, kwa kuonesha ukomavu katika hisia, kwa kutokumbatia wala kukumbatiwa na malimwengu na hatimaye, kuonesha moyo wa umoja na mshikamano katika huduma. Upadre ni daraja la huduma kwa ajili ya Fanmilia ya Mungu na matunda ya kazi hii yanategemea kwa kiasi kikubwa mshikamano walio nao na Kristo mwenyewe ambaye ni kichwa cha Fumbo la Mwili wake, yaani Kanisa. Ni matunda yanayotegemea jinsi ambavyo waliweza kumwilisha tunu mbali mbali katika mchakato wa majiundo yao ya Kipadre.

Majandokasisi wanapaswa kutambua changamoto zinazowakabili Mapadre katika maisha na utume wao, ili kuwa tayari kukabiliana nazo katika azma ya Uinjilishaji Mpya. Waseminari waige mifano bora ya maisha na utume wa Kipadre, waendelee kujielekeza katika utakatifu wa maisha kwa kumpenda Kristo na jirani zao kama njia ya kulijenga na kuliimarisha Kanisa!

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.