2014-06-06 08:32:23

Njoo Roho Mtakatifu!


Kumsadiki Roho Mtakatifu ni kukiri Nafsi ya tatu ya Fumbo la Utatu Mtakatifu, atokaye kwa Baba na Mwana na anayeabudiwa na kutukuzwa pamoja na Baba na Mwana. Huyu ndiye Roho Mtakatifu aliyetumwa mioyoni mwa waamini, ili kupokea uzima mpya wa wana wateule wa Mungu. RealAudioMP3

Katika Fumbo la Utatu Mtakatifu usiogawanyika, Mwana na Roho ni Nafsi tofauti lakini hawatenganiki. Tangu mwanzo hadi mwisho wa nyakati, Baba anapomtuma Mwanaye, anamtuma pia Roho wake anayewaunganisha na Kristo kwa imani ili waamini wakiwa wamefanywa waana waweze kumwita Mungu, Abba, yaani Baba.

Siku hamsini baada ya ufufuko wake nidyo Siku kuu ya Pentekoste, Yesu Kristo aliyetukuzwa mbinguni alimmimina Roho Mtakatifu pasi na kipimo, akamdhihirisha kuwa Nafsi ya Kimungu, hivi kwamba, Fumbo la Utatu Mtakatifu limefunuliwa kikamilifu. Utume wa Kristo na ule wa Roho Mtakatifu vilikuwa utume wa Kanisa, lililopelekwa litangaze na kueneza Fumbo la Umoja wa Utatu Mtakatifu.

Kwa ufupi, Roho Mtakatifu anajenga, anahuisha na kutakasa Kanisa. Roho Mtakatifu anawarudishia Wabatizwa hali ya kufanana na Mungu iliyopotezwa kwa njia ya dhambi na anawafanya waishi ndani ya Kristo uzima uleule wa Fumbo la Utatu Mtakatifu. Anawatuma washuhudie ukweli wa Kristo na kuwapanga katika kazi zao maalum, ili wote wazae tunda la Roho.

Hili ndilo Fumbo ambalo linatarajiwa kuadhimishwa na Baba Mtakatifu Francisko katika Siku kuu ya Pentekoste, Jumapili ijayo kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kuanzia saa 4:00 asubuhi kwa saa za Ulaya, kadiri ya taarifa iliyotolewa na Monsinyo Guido Marini Mshereheshaji mkuu wa Ibada za Kipapa.








All the contents on this site are copyrighted ©.