2014-06-06 09:53:00

Mshikamano na familia maskini!


Baraza la Maaskofu Katoliki Zimbabwe linawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuunganisha nguvu zao, ili kujenga umoja na mshikamano, tayari kusaidia familia zinazoteseka kutokana na myumbo wa uchumi wa kitaifa. Mshikamano huu, unapaswa kujionesha katika maisha ya kiroho na kimwili. Ni changamoto inayotolewa na Askofu Michael Dixon Bhasera, Rais wa Baraza la Maaskofu katoliki Zimbabwe.

Akizungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Zimbabwe hivi karibuni, Baba Mtakatifu Francisko aliwapongeza Maaskofu kutoka Zimbabwe kwa kuwa karibu na wananchi wao wakati wa shida na raha; kabla na baada ya kupata uhuru na hasa zaidi pale maelfu ya wananchi wa Zimbabwe walipolazimika kuikimbia nchi yao kwa kukata tamaa na kukosa mwelekeo kutokana na machafuko ya kisiasa nchini Zimbabwe yaliyopelekea kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Watu wengi walipoteza maisha na kwa hakika watu walimwaga machozi.

Zimbabwe ni nchi ambayo ilikuwa imefikia kiwango kikubwa cha maendeleo lakini machafuko ya kisiasa, yamevuruga maendeleo ya kiuchumi kiasi kwamba, wananchi wengi bado wanaogelea katika dimbwi la umaskini; mmong'onyoko wa kimaadili na hali ya kukata tamaa. Yote haya ni mambo yanayojikita katika miundo inayojikita katika dhambi binafsi na dhambi jamii. Kumbe, kuna haja ya wananchi wa Zimbabwe kufanya toba na wongofu wa ndani kwa kuchuchumilia utakatifu wa maisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.