2014-06-05 15:54:27

Umoja na utume wa Kanisa ni nyenzo muhimu katika maisha ya Kanisa


Patriaki Aram wa kwanza wa Kanisa la Kitume la Armenia amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa moyo wa upendo, urafiki na udugu na kwamba, hii ni mara yake ya tatu kutembelea Vatican na kuonana na Mapapa tangu mwaka 1997, kielelezo cha mshikamano katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene kati ya Makanisa haya mawili.

Kuanguka kwa utawala wa Armenia kunako mwaka 1375 kumepelekea makundi makubwa ya wananchi wa Armenia kuikimbia nchi yao na kujikuta wameenea sehemu mbali mbali za dunia, changamoto ya kuendeleza majadiliano ya kiekumene kati ya Makanisa ili kukabiliana na changamoto za kichungaji, ili hatimaye, umoja kati ya Wakristo uweze kuonekana wazi na Kanisa kutoa ushuhuda wa pamoja. Kanisa la Kitume la Armenia litaendeleza majadiliano ya kitaalimungu na Makanisa mengine duniani, kwani umoja na utume wa Kanisa ni mambo yanayoshibana.

Patriaki Aram wa kwanza amempongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa kujisadaka katika kuwatangazia Maskini Habari Njema ya Wokovu pamoja na kuendelea kutetea utu na heshima ya binadamu, kielelezo cha ushuhuda wa kimissionari, changamoto kubwa kwa Kanisa kwa nyakati zote. Haki na amani ni changamoto nyingine inayopewa kipaumbele cha pekee na Baba Mtakatifu Francisko na hili pia amempongeza kwa juhudi hizi.







All the contents on this site are copyrighted ©.