Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kufungua na kushiriki kikamilifu katika mchakato
wa maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani. Mwaka huu utafunguliwa rasmi hapo tarehe
30 Novemba 2014 Domenika ya kwanza ya Kipindi cha Majilio na kufungwa rasmi tarehe
2 Februari 2016, siku ya Watawa Duniani.
Haya yamebainishwa
katika mkutano wa Wakuu wa Mashirika ya Kitawa uliofanyika hivi karibuni mjini Roma
kwa kuongoza na kauli mbiu “kuuamsha ulimwengu. Watawa katika utume wa Kanisa la leo.”
Wakuu wa Mashirika wametakiwa kuendelea kuzifanyia kazi changamoto na ushauri uliotolewa
na Baba Mtakatifu Francisko wakati alipokutana na kuzungumza na wakuu wa mashirika
ya kitawa na kazi za kitume.
Wakuu wa Mashirika wanaendelea kuchangamotishwa
kufanya mabadiliko makubwa katika maisha na utume wa Mashirika yao kwenye Makanisa
mahalia, kwa kutoa ushuhuda wenye mvuto na mashiko, hasa wanapotembelea nyumba za
mashirika yao kadiri ya sheria na kanuni za Kanisa. Wamekubaliana kwamba, watachangia
tafakari ya kina kuhusu maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya familia
itakayoadhimishwa mwezi Oktoba, mjini Vatican pamoja na kutoa mwelekeo wa maadhimisho
ya Mwaka wa Watawa Duniani: 2014 – 2016.
Maandalizi haya yanafanyika katika
awamu kuu tatu: sehemu ya kwanza ni maadhimisho yatakayofanywa katika ngazi ya Kanisa
la Kiulimwengu kwa ajili ya Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. Maadhimisho haya
yatakwenda sanjari na mikakati itakayopangwa na wakuu wa Mashirika na baadaye maadhimisho
yatayofanyika kwenye Makanisa mahalia kwa kuyahusisha Mashirika ya Kitawa na Kazi
za Kitume katika maeneo yao.
Ratiba elekezi iliyotolewa na Baraza la Kipapa
la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume inaonesha kwamba, tarehe 29 Novemba 2014
kutafanyika kesha la sala kwa ajili ya kuzindua Mwaka wa Watawa Duniani. Tarehe 30
Novemba 2014, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, Baba Mtakatifu Francisko
anatarajiwa kufungua Mwaka wa Watawa Duniani kwa Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa
kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.
Wakati wa Juma la kuombea Umoja wa Wakristo
kuanzia tarehe 22 hadi tarehe 24 Januari 2015 kutafanyika kongamano la kiekumene kimataifa
kwa kuwaalika watawa kutoka Mashirika mbali mbali ya kitawa nje ya Kanisa Katoliki.
Tarehe 8 hadi tarehe 11 Aprili 2015 kutafanyika kongamano la kimataifa kwa ajili ya
walezi katika maisha ya kuwekwa wakfu, lengo ni kubainisha vigezo vinavyoibuliwa katika
tasaufi ya maisha ya pamoja.
Tarehe 23 hadi tarehe 26 Septemba 2015 kutafanyika
kongamano la watawa vijana. Juma la maisha ya kitawa litaadhimishwa kuanzia tarehe
24 Januari hadi tarehe 2 Februari 2016 na hapo Baba Mtakatifu atafunga rasmi Mwaka
wa Watawa Duniani. Kwa ujumla hii ndiyo ratiba elekezi itakayotumika kwa ajili ya
Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani 2014 hadi mwaka 2016.
Imehaririwa na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.