2014-06-05 08:19:11

Lindeni na kutetea uhuru wa kidini!


Baba Mtakatifu Francisko anawaomba waamini wa Makanisa ya Kiorthodox na Kikatoliki Barani Ulaya, kusimama kidete kulinda na kutetea uhuru wa kidini, kwa kuheshimiana na kuthaminiana kama ndugu wamoja katika Kristo, ili kuwamegea wengine matumaini katika maisha.

Huu ni ujumbe kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko aliowandakia wajumbe wanaoshiriki katika Jukwaa la nne la majadiliano ya kiekumene kati ya Waorthodox na Wakatoliki, majadiliano yaliyofunguliwa hapo tarehe 2 na yanafungwa rasmitarehe 6 Juni 2014, kwa kuongozwa na kauli mbiu "Dini natofauti za kitamaduni: changamoto kwa Makanisa Barani Ulaya". Jukwaa hili limeandaliwa na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya kwa kushirikiana na Makanisa ya Kiorthodox yaliyoko Barani Ulaya.

Ujumbe huu umeandikwa na Kardinali Pietro Parolin Katibu mkuu wa Vatican kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko anayewapongeza wahusika wakuu kwa kuendeleza jitihada za majadiliano ya kiekumene kati ya Makanisa, ili kuimarisha umoja na mshikamano, ili kulinda na kutetea uhuru wa kidini, kwa kuheshimiana na kuthaminiana. Mkutano huu unaendelea kujadili masuala ya kibinadamu, mikakati ya kichungaji, masuala ya kijamii na kimaadili.

Mkutano huu unafanyika kwa faragha kwa kuangalia kwa namna ya pekee masuala ya kidini na tamaduni Barani Ulaya; tunu msingi za maisha ya Kikristo na umuhimu wake katika jamii ya nyakati hizi; uhuru wa kidini, mchango wa Makanisa katika kukuza na kuendeleza hekima ya Kikristo pamoja na majadiliano ya kidini yanayopania ujenzi wa misingi ya maadili na utu wema miongoni mwa wananchi wa Bara la Ulaya. Jukwaa hili linahudhuriwa na viongozi waandamizi kutoka Kanisa la Kiorthodox na Kanisa Katoliki.

Wajumbe wanaendelea kukazia umuhimu wa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu; wamewaombea wananchi wa Ukraine wanaokabiliana na machafuko ya kisiasa kwa wakati huu. Kuna haja ya kuheshimiana hata katika tofauti zinazojitokeza katika masuala ya kidini na kitamaduni, kwani Bara la Ulaya lina utajiri mkubwa wa watu kutoka katika kabila, lugha na jamaa; wote hawa wanahistoria, lugha na tamaduni zao. Changamoto za Kikristo hazipanii kung'oa tamaduni za watu, bali kuwasaidia watu kujitamadunisha zaidi kwa kuzingatia kweli za Kiinjili.







All the contents on this site are copyrighted ©.