2014-06-04 07:34:04

Umuhimu wa Sinodi katika maisha na utume wa Kanisa


Askofu Fabio Fabene, Katibu mkuu msaidizi wa Sinodi za Maaskofu katika mahojiano maalum na Gazeti la L’Osservatore Romano anasema kwamba, Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kutoa kipaumbele cha pekee katika kudumisha umoja na mshikamano ndani ya Kanisa kwa kukazia umuhimu wa Sinodi za Maaskofu katika maisha na utume wa Kanisa. RealAudioMP3

Kutokana na dhamana hii nyeti ndani ya Kanisa ndiyo maana Baba Mtakatifu Francisko, tarehe 30 Mei 2014 amemweka wakfu Askofu Fabio Fabene katika Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.

Askofu Fabene alianza utume wake mjini Vatican kunako mwaka 1997 na tarehe 8 Februari 2014 akateuliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa katibu mkuu msaidizi wa Sinodi za Maaskofu. Anakumbuka mchango mkubwa uliofanywa na Marehemu Kardinali Bernardin Gantin katika Baraza la Kipapa la Maaskofu kwa kukazia tunu msingi za maisha ya kifamilia na ushirikiano katika kutekeleza majukumu mbali mbali ndani ya Baraza.

Hii ndiyo changamoto anayotaka kuifanyia kazi katika utekelezaji wa majukumu yake kwa kuhakikisha kuwa, Sinodi za Maaskofu zinakuwa ni kama Familia. Baraza la Maaskofu limejitahidi kuangalia na hatimaye kupitisha Katiba za Mabaraza ya Maaskofu kadiri ya miongozo iliyotolewa na Mama Kanisa na kwamba, Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa kichungaji Injili ya Furaha, “Evangelii gaudium” anakazia kwa namna ya pekee umoja na mshikamano katika maisha na utume wa Kanisa.

Askofu Fabio Fabene si mgeni sana katika kuta za Vatican, kwani wakati wa mchakato wa kumtafuta kiongozi mpya wa Kanisa Katoliki baada ya Baba Mtakatifu Benedikto XVI kung’atuka kutoka madarakani alishirikiana kwa karibu zaidi na Kardinali Lorenzo Baldiselli, kumbe, kama Katibu wa Sinodi za Maaskofu anapenda kushirikisha mang’amuzi na uzoefu wake kutoka katika Baraza la Kipapa la Maaskofu.

Mtumishi wa Mungu Papa Paulo VI kunako tarehe 15 Septemba 1965 alianzisha maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu kama kielelezo makini cha umoja na mshikamano miongoni mwa Maaskofu katika utekelezaji wa dhamana ya kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza watu wa Mungu. Haya ndiyo mambo makuu ambayo Baba Mtakatifu Francisko anapenda kuyaona yakitendeka ndani ya Kanisa wakati wa maadhimisho ya Sinodi za Maaskofu Katoliki.

Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu Familia itakayoadhimishwa mwezi Oktoba, 2014 mjini Vatican itaangalia fursa, matatizo na changamoto zinazoendelea kuikabilia familia ya mwanadamu. Wanafamilia watapewa nafasi ya kujadili kuhusu mustakabali wa maisha na utume wao ndani ya Kanisa, ili hatimaye, kuwasaidia Maaskofu kutoa mapendekezo yatakayofanyiwa kazi na Baba Mtakatifu, ili kweli Kanisa liweze kuendelea kutangaza Injili ya Familia katika ulimwengu mamboleo.

Mchakato wa maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kuhusu familia unaendelea vyema. Baba Mtakatifu anaitaka Familia ya Mungu kuwajibika barabara katika kutangaza Injili ya Familia. Kila Askofu mahalia anatambua dhamana na utume wake kwa Kanisa mahalia lakini pia anaungana na Kanisa zima kwa ajili ya ustawi na mafao ya Familia ya Mungu. Hii ni changamoto kubwa kutoka katika Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Maaskofu kama wachungaji wakuu wa Makanisa mahalia wanapaswa kuwa watu na wajenzi wa umoja na mshikamano, ili kuchangia ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo. Sinodi za Maaskofu zinalenga kuimarisha na kukuza umoja na mshikamano kati ya Maaskofu!








All the contents on this site are copyrighted ©.