Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa katika maadhimisho ya Siku kuu ya Moyo Mtakatifu
wa Yesu hapo tarehe 27 Juni 2014 kutembelea Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu
wa Yesu, kilichoko mjini Roma sanjari na maadhimisho ya siku 90 ya Chuo Kikuu cha
Kikatoliki.
Kardinali Pietro Parolin katika barua aliyomwandikia Kardinali
Angelo Scola, Rais wa Taasisi ya Gemeli Toniolo anasema, Baba Mtakatifu Francisko
anaendelea kuwahimiza wadau mbali mbali kushirikiana kwa dhati katika kuimarisha Chuo
Kikuu cha Kikatoliki, kwa ajili ya mafao ya wengi. Anatambua mchango unaotolewa na
Kitivo cha tiba na upasuaji kilichoko Hospitali ya Gemelli wakati huu kinaposherehekea
Jubilee ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.
Kitivo hiki kimeendelea kuwa ni
msaada mkubwa kwa ajili ya tiba kwa wagonjwa kwa kuthamini na kuheshimu utu wa binadamu.
Kutokana na mchango huu, Baba Mtakatifu Francisko amekubali mwaliko wa kutembelea
Hospitali ya Gemelli ili kuzungumza na wafanyakazi pamoja na kusalimiana na wagonjwa
wanaolazwa Hospitalini hapo.
Kardinali Angelo Scola katika ujumbe wake kama
sehemu ya maandalizi ya tukio hili amewaandikia wanafunzi wa kitivo cha tiba na upasuaji
cha Chuo Kikuu cha Moyo Mtakatifu wa Yesu, kutokubali kamwe kupokonywa matumaini yao
na wala wasithubutu kutafuta njia za mkato katika maisha, bali waoneshe ujasiri wa
kupambana na magumu pamoja na changamoto za maisha kwa kujikita katika majiundo makini
ya kitaaluma na tafiti mbali mbali.
Tangu kuanzishwa kwake, Chuo Kikuu cha
Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu kimekuwa ni mtekelezaji mkuu wa utume wa Kanisa
katika kuwafunda vijana taaluma sanjari na kuendeleza mchakato wa majadiliano kati
ya imani na uwelewa wa mwanadamu, ili kuwapatia vijana wa kizazi kipya ufahamu makini
kwa kujichotea hekima na busara kutoka kwa Yesu Kristo, chemchemi na busara yote ya
kimungu katika maisha ya mwanadamu!