2014-06-04 06:54:23

Mwaka wa Mtumishi wa Mungu Padre Schneider


Masista wa Maria Imakulata wanapenda kuwakaribisha ninyi nyote wanapotafakari mwaka wa Mtumishi wa Mungu Padre Yohane Schneider ambao ulifunguliwa rasmi tarehe 07-12-2013 na utafungwa tarehe 07-12-2014 ukiongozwa na kauli mbiu “kuiishi karama ya mwanzilishi katika mazingira tunamoishi na kufanya kazi”. RealAudioMP3

Huu ni mwaliko ambao unatupatia nafasi ya kutafakari zaidi na kwa kina maisha ya Mtumishi wa Mungu, baba mwanzilishi wetu Padre Yohane Schneider. Hakika Maisha ya mwanzilishi wetu ni chachu ya maisha yetu.

Shirika la Maria Imakulata lilianzishwa mnamo mwaka 1854 huko Wroclaw, nchini Poland, na Mtumishi wa Mungu Padre Yohane Schneider. Shirika lilisajiliwa na kupata hati ya Kipapa tarehe 22 Desemba 1897 lilithibitishwa na hatimaye kupewa Hati ya Sifa. Hivyo tunapokumbuka miaka 160 tangu kuanzishwa kwa Shirika letu tumeona ni vema kama familia moja ya Wana Immakulata kukaa chini na kutafakari fadhili ambazo Mungu anatukirimia siku kwa siku bila ya mastahili yetu. Kwetu imekuwa ni tendo la shukrani kwa Mungu kwa wema na upendo wake kwetu sisi Watawa wa Shirika la Immakulata.

“Saidieni kuokoa roho za mabinti zilizo karibu na genge la uharibifu...” ni wosia wa mwanzilishi wetu ambao ndio maneno ya msingi katika Karama ya Shirika letu, yaani kuwasaidia wasichana na akina mama walio na maisha duni ili waweze kumtambua Mungu na kuuishi utu na Ukristo wao kwa kutimiza wajibu na majukumu yao ndani ya jamii katika misingi ya haki na upendo.

Kwa njia hiyo, mbegu ya Shirika letu ilipandwa na hatua kwa hatua Shirika linaendelea kukua na kusambaa katika mabara na nchi mbalimbali duniani. Masista wa Maria Immakulata wanafanya kazi katika Bara la Ulaya, Asia na Afrika; katika bara la Afrika tupo Tanzania na tunafanaya kazi katika Jimbo katoliki la Tunduru- Masasi katika Parokia ya Chikukwe ambamo ipo nyumba ya malezi ya Wanovisi.

Pia tunafanya kazi katika Parokia ya Nanjota na ipo nyumba ya malezi ya wakandidati na wapostulanti. Katika Jimbo kuu la Dar es Salaam tunafanya kazi katika Parokia ya Kurasini na ndipo ilipo nyumba Mama ya Shirika katika kanda ya Tanzania. Baadhi ya Masista wanafanya kazi katika ubalozi wa Vatican nchini Tanzania.

Vilevile tunafanya kazi katika Jimbo la Same katika Parokia ya Mwanga na pale ni Kituo cha kiroho na kielimu kwa Masista wetu. Pia tunafanya kazi katika Parokia ya Kilomeni. Kwa jinsi hiyo, tunaweza kusema siri kuu ya mafanikio yetu ni Sala na Kazi ambamo tunakutana na Kristo mpole, mnyenyekevu na mwenye huruma, tunapotoa huduma kwa wazee, akina mama, vijana, maskini, wagonjwa na watoto, pia tupofundisha dini shuleni na utume wetu Parokiani. Hivyo basi, tunapoendelea kumshukuru Mungu naweza kusema kwamba: Zawadi ya sala yetu ni Amani, Upendo na Furaha, kwani mikono yetu tunaitumia kwa kazi, na mioyo yetu tunaiinua kwa Mungu.

Miito ya kitawa:
Shirika la Masista wa Maria Imakulata linapokea wasichana wote wenye wito na utayari wa kuokoa Roho zilizopo katika genge la uaribifu ambao wana elimu yoyote yaani baada ya darasa la saba.

Je unapenda kujiunga nasi?

Tuandikie
Murugenzi wa Miito
Shirika la Masista wa Maria Imakulata
S. L. P 47, Same.
Kilimanjaro-Tanzania.








All the contents on this site are copyrighted ©.