Jubilee ya miaka 25 ya uhusiano wa Kidiplomasia kati ya Vatican na Poland
Uhuru na mshikamano ni mambo msingi wakati huu Poland na Vatican zinapofanya kumbu
kumbu ya Jubilee ya Miaka 25 tangu nchi hizi mbili zilizpoanzisha uhusiano wa Kidiplomasia,
mambo muhimu pia wakati huu wa mabadiliko makubwa katika medani za kisiasa na kijamii.
Mabadiliko makubwa yaliyofanywa na Poland katika historia ya miaka ya hivi
karibuni ni kielelezo makini cha utashi wa wananchi wa Poland kutaka mabadiliko ya
dhati yanayojikita katika uhuru na mashikamano wa kweli, hali iliyopelekea kuanguka
kwa ukuta wa Berlin, hapo ukawa ni mwanzo mpya wa maisha ya wananchi wa Poland.
Hii
ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican
wakati wa maadhimisho ya Jubilee ya miaka 25 ya uhusiano wa kidiplomasia kati ya Poland
na Vatican, huko Varsavia. Uhuru wa kidini ni mwendelezo wa mambo msingi katika maisha
ya wananchi wa Poland yanayojionesha katika katiba na Sheria za Kimataifa.
Uhuru
wa kidini ni jambo ambalo limeendelea kupewa kipaumbele cha pekee katika mabadiliko
yanayojitokeza nchini Poland, ili kuwawezesha watu kujenga misingi ya imani na matumaini
thabiti sanjari na utekelezaji wa demokrasia ya kweli dhidi ya vitendo vya kutovumiliana,
ubaguzi na misimamo mikali ya kidini, mambo ambayo yanapaswa kukemewa na kuoneshwa
kwamba, hayafai kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya binadamu.
Kanisa linaheshimu
na kuthamini kazi zinazotekelezwa na Serikali na kwamba, ushiriki wake katika ustawi
na maendeleo ya wananchi wa Poland unajikita katika uhuru wa kuabudu pamoja na utekelezaji
wa haki msingi za binadamu, ili kudumisha amani na utulivu. Utekelezaji wa uhuru wa
kuabudu kwa namna ya pekee unahitaji kuongozwa na kanuni auni na mshikamano.
Katika
ziara yake ya kichungaji nchini Poland, Kardinali Pietro Paroli tarehe 1 Juni 2014
ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kama kielele cha Jubilee ya miaka 25 ya uhusiano
wa Kidiplomasia kati ya Poland na Vatican; ibada ambayo imehudhuriwa pia na viongozi
wa Kanisa na Serikali kutoka Poland. Amewakumbusha waamini kwamba, ushindi wa uhuru
wa kidini umepatikana kwa njia ya Msalaba. Kumbe, hakuna sababu ya kuwa na wasi wasi,
licha ya ukosefu wa fursa za ajira, tatizo la watu kukimbia nchi yao na watu kutokuwa
na uhakika wa maisha yao kwa siku za usoni, mambo ambayo yanayumbisha tunu msingi
za maisha ya ndoa na familia.
Kardinali Pietro Parolin anawataka wananchi wa
Poland kujiweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Mtakatifu Yohane Paulo II, ili kwa
maombezi yake, Mwenyezi Mungu aendeleee kutekeleza mpango wake kwa ajili ya familia
ya binadamu. Mtakatifu Yohane Paulo II anaweza kuitwa kuwa ni msimamizi wa uhuru wa
wananchi wa Poland.