2014-06-03 07:16:27

Watangazieni watu Injili ya Matumaini!


Hija za kitume zinazofanywa na Maaskofu Katoliki mjini Vatican walau kila baada ya miaka mitano, zinalenga kuimarisha moyo wa sala, umoja na mshikamano na Khalifa wa Mtakatifu Petro pamoja na kuendelea kujipyaisha katika maisha ya kiroho. Zimbabwe ni kati ya Nchi ambazo ziko Kusini mwa Bara la Afrika, iliyofanikiwa kukuza na kuimarisha ari na moyo wa kimissionari, kiasi cha watu kujisadaka kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa nchini Zimbabwe.

Leo hii, Kanisa linaendelea kuvuna matunda ya sadaka hii kutoka nchini Zimbabwe. Matunda haya yanajionesha kwa namna ya pekee katika huduma zinazotolewa na Kanisa katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu! Zimbabwe imebahatika kuwa na idadi kubwa ya miito mitakatifu na kwamba, miito hii inaendelea kukua na kuchanua, kielelezo cha neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu, licha ya changamoto zinazojitokeza, mwaliko wa kuendelea kudumu katika sala ya shukrani.

Hii ni sehemu ya hotuba iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 2 Juni 2014 wakati alipokutana na kuzungumza na Baraza la Maaskofu Katoliki Zimbabwe linalofanya hija yake ya kitume mjini Vatican. Baba Mtakatifu anawapongeza Maaskofu kwa kusimama kidete kulinda na kuwatetea wanyonge, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum. Watu wanaendelea kuteseka: kiroho, kimwili na kimaadili kutokana na kushamiri kwa uwepo wa miundo ya dhambi, mwaliko wa kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu kwa kujikita katika maadili.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika kwa namna ya pekee Maaskofu Katoliki nchini Zimbabwe kujibidisha katika ujenzi wa umoja na uponyaji wa kitaifa katika medani mbali mbali za maisha zinazoundwa na makundi ya watu nchini humo, ili kweli umoja uweze kujidhihirisha tena kwa kuendeleza mchakato wa upatanisho wa kitaifa unaojikita katika upendo kwani uponyaji ni neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu anasema, wananchi wengi wa Zimbabwe wana madonda makubwa, kiasi cha kuwakatisha tamaa. Kumbe, ni dhamana ya Maaskofu kuhakikisha kwamba, wanawajengea wananchi wa Zimbabwe matumaini mapya kwani Kristo ameshinda dhambi na mauti na mwanga daima utatawala katika maisha ya watu. Kanisa litaendelea kutangaza Injili ya Matumaini nchini Zimbabwe, kwa wale waliopondeka na kuvunjika moyo, ili waweze kuonja tena msamaha na huruma ya Mungu kwa njia ya Sakramenti za Kanisa hasa Sakramenti ya Upatanisho na Ekaristi Takatifu chanzo na kilele cha maisha ya Kikristo.

Baba Mtakatifu anawataka viongozi wa Kanisa kuonesha unyenyekevu kwa Roho Mtakatifu kwa kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano na Mapadre wao sanjari na kutafuta na kukuza miito mitakatifu. Maaskofu waendelee kuwasindikiza Mapadre vijana katika maisha na wito wao wa Kipadre; kwa kuwasaidia katika kuhibiri na kuishi kadiri ya kweli za Kiinjili, imani na mapendo kwa Mungu. Mapadre wajifunze kujisadaka na kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya jirani zao, kwa kuonesha matumaini ya kinabii katika haki nchini Zimbabwe.

Baba Mtakatifu anasema, ustawi na maendeleo ya Kanisa nchini Zimbabwe na Afrika katika ujumla wake kwa namna ya pekee kabisa unategemea majiundo makini kwa waamini walei; Mapadre watakatifu pamoja na Makatekista waliofundwa kikamilifu wanaotolea ushuhuda amini wa maisha yao ya Kikristo katika jamii inayowazunguka. Watawa wasaidiwe kuitakatifuza Zimbabwe kwa njia ya upendo kwa Mungu na jirani zao. Wanandoa watarajiwa waandaliwe kikamilifu kwa kuwashirikisha utajiri unaobubujika kutoka katika Mafundisho adili ya Kanisa pamoja na upendo, ili waweze kuishi katika furaha na uhuru wa kweli kama Baba na Mama.

Baba Mtakatifu Francisko, mwishoni, amewataka Maaskofu Katoliki kutoka Zimbabwe kuwaimarisha ndugu zao katika imani na umoja na kwamba, Khalifa wa Mtakatifu Petro yuko pamoja nao katika kulihudumia Neno la Mungu, ili kweli Wakristo nchini Zimbabwe waweze kuwa ni chumvi na mwanga wa mataifa Barani Afrika na duniani kote.







All the contents on this site are copyrighted ©.