2014-06-03 11:50:19

Wamissionari waliotekwa nyara wako katika hali nzuri!


Kardinali Fernando Filoni, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu wakati wa ziara yake ya kikazi nchini Cameroon amekutana na kuzungumza na Wamissionari watatu waliokuwa wametekwa nyara kwa takribani mwezi mmoja na hatimaye kuachiliwa huru, Jumapili tarehe 1 Juni 2014. Kardinali Filoni anamshukuru Mungu kwa zawadi hii kubwa kwa ajili ya Kanisa la Cameroon, ambalo lilikosa huduma za kiroho na kiutu zilizokuwa zinatolewa na Wamissionari hawa nchini Cameroon.

Wamissionari waliokuwa wametekwa nyara ni kutoka katika Shirika la Zawadi ya Roho Mtakatifu, Fidei Donum: Padre Gianantonio Allegri na Padre Giampaolo Marta wote wawili kutoka Italia pamoja na Sr. Gilberte Bussier kutoka Canada. Mapadre hawa wako katika hali nzuri: kisaikolojia na kiafya na kwamba, wamesaidiana wakati wote walipokuwa wametekwa, lakini zaidi, wameonja uwepo wa Kanisa zima kwa njia ya mshikamano wa sala na sadaka, kiasi kwamba, wakaendelea kuwa na imani thabiti licha ya hofu na mashaka kuhusu hatima ya maisha yaliyokuwa mikononi mwa watekaji nyara.

Serikali ya Cameroon bado inaendelea kufanya uchunguzi wa kina ili kubainisha wale waliohusika na utekaji nyara huo, ili waweze kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.







All the contents on this site are copyrighted ©.