Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis,
tarehe 16 Oktoba 2014 wakati wa maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani, litatoa tuzo
mbili zenye thamani ya Euro 10, 000 kwa kila kundi la wanawake ambalo limejifunga
kibwebwe kuhakikisha kwamba, baa la njaa linapewa kisogo katika maisha yao.
Tuzo
hii inakwenda sanjari na kampeni inayoongozwa na kauli mbiu “Wanawake ni vyombo vya
maendeleo”, iliyozinduliwa hapo tarehe 8 Machi 2014 katika maadhimisho ya Siku ya
Wanawake Duniani. Wanawake sehemu mbali mbali za dunia wamekuwa daima mstari wa mbele
katika mapambano dhidi ya baa la njaa kwa kujikita katika uzalishaji wa mazao ya chakula
kwa ajili ya familia zao na mazao ya biashara ili kujipatia uwezo wa kiuchumi.
Wachunguzi
wa masuala ya wanawake na maendeleo wanasema kwamba, kuna wakati wanawake wanawajibika
kufanya maamuzi machungu katika maisha yao kwa kuamua ni mtoto yupi apewe chakula
wakati wa baa la njaa kama inavyojionesha nchini Syria na Sudan ya Kusini.
Wanawake
waliojengewa uwezo katika uzalishaji wa mazao ya chakula na kilimo wamekuwa ni mfano
wa kuigwa katika matumizi ya teknolojia rafiki kwa ajili ya kulinda na kutunza mazingira.
Caritas Internationalis inaendesha kampeni dhidi ya baa la njaa duniani inayoungwa
mkono na Baba Mtakatifu Francisko, ili watu waguswe na mahangaiko ya jirani zao!